1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

TEHRAN: Mgogoro wa nyuklia wa Iran kujadiliwa karibuni

17 Juni 2007
https://p.dw.com/p/CBr3

Majadiliano kati ya mkuu wa sera za nje,wa Umoja wa Ulaya,Javier Solana na mpatanishi mkuu wa Iran,Ali Larijani kuhusu mradi wa nyuklia wa Iran,yatafanywa katika kipindi cha siku chache zijazo.Msemaji wa wizara ya masuala ya nje wa Iran,Mohammed Ali Hosseini,alitamka hayo kwenye mkutano wake wa kila juma pamoja na waandishi wa habari mjini Tehran.Lakini hakutoa maelezo zaidi kuhusu tarehe au wapi mkutano huo utafanywa.Kwa upande mwingine,Larijani amesema,majadiliano yake pamoja na Solana mwezi uliopita yalikuwa ya busara.Akaongezea kuwa pande zote mbili zinapaswa kuchukua hatua sahihi zikiwa na mwelekeo wa mantiki na kuzuia kupitishwa kwa azimio la tatu la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa,kuhusika na mradi wa nyuklia wa Iran uliozusha mabishano.