1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

TRIPOLI:Ufaransa yahidi kuimarisha uhusiano na Libya

26 Julai 2007
https://p.dw.com/p/CBfF

Rais wa Ufaransa Nicolaus Sarkozy ameahidi kuimarisha uhusiano na Libya, kufuatia hatua ya nchi hiyo kuwaachia wauguzi watano wa Bulgaria na daktari mmoja wa Kipalestina.

Rais huyo wa Ufaransa aliyasema hayo baada ya kukutana na mwenyeji wake kiongozi wa Libya Kanali Muhamar Gaddafi katika siku ya kwanza ya ziara yake nchini Libya.

Nchi hizo mbili pia zilitia saini makubaliano ya kushirikiana katika nyanja mbalimbali zikiwemo za kiulinzi, afya, vita dhidi ya ugaidi pamoja na nishati ya nuklia kwa matumizi ya kawaida.

Libya inategemea kuimarisha ushirikiano na nchi za magharibi kufuatia hatua yake ya kuwaruhusu wauguzi hao kutumikia kifungo cha maisha nchini mwao.Wauguzi hao walikuwa wakikabiliwa na makosa ya kuwaambukiza zaidi ya watoto 400 nchini Libya virusi vya ukimwi.

Mjini Washington, Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo Condoleza Rice amesema kuwa anapanga kuzuru Libya hivi karibuni ikiwa ni ishara ya kuimarika kwa uhusiano kati ya nchi hizo mbili.

Umoja wa Ulaya umetangaza kuchangia katika mfuko ulioanzishwa na Libya kwa ajili ya fidia kwa familia za wahanga.

Wakati huo huo,Libya imepinga hatua ya Rais wa Bulgaria Georgy Parvanov kutoa msamaha kwa wauguzi hao mara baada ya kurejea nchini mwao.

Libya imesema kuwa hatua hiyo ni kinyume na mkataba wa ushirikiano kati ya nchi hizo uliyotiwa saini mwaka 1984, ambao hautoi nafasi kwa watu waliyofanya uhalifu ugenini kusamehewa wanaporudishwa kwao kutumikia adhabu.