1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump aelekea Saudi Arabia

19 Mei 2017

Rais wa Marekani Donald Trump anasafiri kuelekea Ghuba katika ziara yake ya kwanza kabisa ya nje ya nchi tangu achukue hatamu za uongozi.

https://p.dw.com/p/2dE6t
USA Donald Trump steigt in die Air Force One
Picha: Reuters/J. Ernst

Tangu Rais Jimmy Carter, Trump ndiye rais wa kwanza kufanya ziara yake yake ya kwanza mbali na nchi za karibu kama Mexico na Canada. Anaanza kwa kuizuru Saudi Arabia, eneo lililo mbali kabisa na matatizo mengi ya nyumbani. Ziara hiyo ya rais wa Marekani huko Saudi Arabia itashuhudia kutiwa saini mkataba wa dola bilioni 100 wa silaha baina ya nchi hizo mbili.

Elliot Abraham ni afisa kutoka baraza lenye ushawishi mkubwa la masuala ya nchi za nje, "ni jambo la kuridhisha, kwa sababu wakati wa kampeni za uchaguzi, Donald Trump alizungumzia kuhusiana na Marekani kujiondoa kutoka kwenye mizozo yote ya Mashariki ya Kati," alisema Elliot, "na sasa ziara yake ya kwanza ya nje ya nchi inashuhudia yeye kuelekea huko huko Mashariki ya Kati."

Viongozi wa Kiarabu walikuwa na matumaini na urais wa Trump

Ikulu ya White House ilisema kwamba Trump anasafiri ili kuuleta pamoja ulimwengu wa Kiislamu dhidi ya maadui. Atakutana na mfalme Salman ibn Abd al-Aziz pamoja na wengine katika familia hiyo ya kifalme na ahudhurie pia mkutano wa mataifa ya Kiarabu. Trump pia atatoa hotuba ya kukashif masuala ya itikadi kali katika mkutano wake na viongozi wa karibu mataifa 50 ya Kiarabu na Kiislamu. Marais wa mataifa hayo walipewa mwaliko maalum mjini Riyadh ili wakutane na rais huyo wa Marekani.

Saudi Arabien König Salman Bin Abdul Aziz Al Saud
Trump atakutana na mfalme wa Saudi Arabia Salman Bin Abdul AzizPicha: Picture alliance/abaca/B. Press

Nile Gardiner kutoka Wakfu wa Urithi wa Kihafidhina, unaoishauri serikali ya Marekani kuhusiana na masuala muhimu ya nchi za kigeni na ndani ya nchi anasema, viongozi katika mataifa ya Kiarabu walikuwa na matumaini makubwa kuhusiana na urais wa Trump licha ya matamshi yake ya kukashif Uislamu wakati wa kampeni na zile juhudi zake za kuweka marufuku ya muda ya mataifa saba ya Waislamu kuingia nchini humo.

"Lengo la ziara hiyo ni kuufufua uhusiano baina ya Marekani na Saudi Arabia na kuwahakikishia Wasaudi Arabia kwamba Marekani iko tayari kutilia kikomo ushawishi wa Iran unaoleta msukosuko katika eneo hilo," alisema Gardiner.

Uhusiano wa Trump na Saudi Arabia utakuwa mtulivu

Gardiner anazidi kusema kwamba, rais wa zamani Barack Obama alizipuuza nchi marafiki wa Marekani katika eneo hilo la Mashariki ya Kati.

USA Barack Obama in Chicago
Barack Obama anashutumiwa na Warepublican kwa kuuharibu uhusiano wa Marekani na Saudi ArabiaPicha: Reuters/K. Krzaczynski

Emma Ashford kutoka taasisi ya libertarian Cato, anasema "Uhusiano wa Trump na Saudi Arabia utakua mtulivu kuliko ulivyokuwa wakati wa Obama, lakini hili halitoi hakikisho kwamba ni jambo zuri kwa sera ya nchi za nje ya Marekani."

Huko Riyadh kinyume na mtangulizi wake bwana Obama alivyofanya mjini Cairo mwaka 2009, Trump hatoielekeza hotuba yake kwa raia wa Kiarabu bali viongozi wao, isitoshe, masuala ya kukiukwa kwa haki za kibinadamu yatajadiliwa faraghani na hii ndiyo inayoonekana kuwa sera ya kigeni ya Trump.

Mwandishi: Alexandra von Nahmen

Tafsiri: Jacob Safari

Mhariri: Mohammed Khelef