1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump akutana na Obama

Sekione Kitojo
11 Novemba 2016

Rais mteule wa Marekani Donald Trump na rais wa sasa Barack Obama waliweka kando uhasama wao wakati walipokutana kwa dakika 90 katika ikulu ya Marekani ya White House mkutano uliolenga kutuliza hofu juu ya demokrasia

https://p.dw.com/p/2SXKf
USA Washington Treffen Obama und Amtsnachfolger Trump
Rais mteule Doland Trump (kushoto) na rais wa sasa Barack Obama (kulia)Picha: Reuters/K. Lamarque

Wakati  maandamano  dhidi  ya rais mteuele  tajiri  mfanyabiashara ya  kuuza  majumba  kutoka  chama  cha  Republican  yalirindima katika  miji  ya  Marekani  na  miji  mikuu  ya  nchi  mbali  mbali duniani  ikitafakari  na  hali  ya  sintofahamu  inayoikabili  dunia, Obama  na  Trump  waliahidi  kuendelea  na utaratibu  usiokuwa  na matatizo  wa  kupokezana  madaraka.

Baada  ya  kampeni  iliyokuwa na  kila  hali  ya  uhasama  ambayo ilimalizika  kwa  kuchaguliwa  kwa  bilioanea  mwenye  umri  wa miaka  70  na nyota  wa  zamani  katika  televisheni ambaye hajawahi  kushika  wadhifa  wa  uongozi  wa  umma  na  ambaye alipata  madaraka  kwa  kampeni  za  sera  za  mrengo  wa  kulia, ujumbe  ulikuwa: mambo  hapa  yanakwenda  kama  kawaida  yake katika  demokrasia.

US Präsident Barack Obama im Rosengarten nach Clintons Wahlniederlage
Rais barack Obama na makamu wake Joe BidenPicha: Picture-Alliance/dpa/M. Reynolds

Rais  anayeondoka  madarakani  na  mrithi  wake walikuwa  na mazungumzo  ya  ana  kwa  ana  katika   ofisi  kuu  ya  rais , Oval Office, kwa  kile  Obama  alichokieleza  kuwa  ni  mazungumzo mazuri, na  tena  alionekana  kuwa  katika  hali  ya  kawaida  kabisa hadharani.

"Nimetiwa  moyo sana  nafikiri na hamasa ya  rais mteule  Trump akitaka kufanyakazi  na  timu  yangu , kuhusu masuala  mengi ambayo  nchi hii  muhimu  inayakabili".

Mkutano  huo  ambao  umekuja  chini  ya  masaa 36 baada  ya ushindi  wa  kushitua  wa  Trump  dhidi  ya  mgombea  wa  chama cha  Democratic  Hillary Clinton, ulikuwa  na  uwezo  wa  kuwa wa shaka  shaka.

Kwa  kuwa , Trump  aliongoza  kile  kinachojulikana  kama  vuguvugu la  uzawa, likipinga  kwamba  Obama  alizaliwa  nchini  Marekani, wazo  ambalo  linaonekana  kuwa  na  dhamira  ya  ubaguzi, na aliachana  na  mtazamo  huo  hivi  karibuni.

Rais  mjivuni

USA | Melania Trump und Michelle Obama
Melania Trump (kushoto) Michelle Obama (kulia)Picha: REUTERS

Na  iwapo  rais mteule  atatekeleza  kila  ahadi  aliyoitoa  wakati  wa kampeni, ataondosha  karibu  kila  mafanikio  ya  Obama  yalipo. Trump  hivi  karibuni  alimuita  Obama , "rais  mwenye majivuno mno katika  historia ya  nchi  hiyo"  , alisema  anamatumaini  ya kupata  ushauri  wa  rais.

"Tumejadiliana  kuhusu  hali  mbali  mbali, baadhi  nzuri  sana  na baadhi  zenye matatizo. Nina  matumaini  makubwa ya  kufanyakazi na  rais  hapo  baadae ikiwa  ni  pamoja  na  ushauri".

Wakati  waume  zao  wakifahamiana , mke  wa  rais , Michelle Obama  pia  alikutana  na  mrithi  wake Melania Trump  ikulu ya White House. makamu  wa  rais Joe Biden , wakati  huo  huo , alikutana  na  mgombea  mwenza  wa  Trump , Mike ence, ambaye ndie  makamu  mpya  wa  rais.

Maandamano  pia  yaliendelea  katika  mitaa  ya  miji  ya  Marekani kupinga  kuchaguliwa  kwa  Doland Trump  kuwa  rais. Katika  pwani ya  mashariki, waandamano  yalifanyika  mjini  Washington, Baltimore, Philadelphia  na  New York , wakati  upande  wa  pwani ya  magharibi  waandmanaji  waliingia  mitaani  mjini  Los Angeles, San Francisco  na  Oakland  ,  Califonia, na  Portland, Oregon. Maandamano  hayo  kwa  kiasi  kikubwa  yalikuwa  ya  amani , licha ya  kuwa  kulikuwa  na  vitendo vya  hapa  na  pale vya  ghasia.

Mwandishi: Sekione Kitojo / afpe / rtre

Mhariri: Daniel Gakuba