1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump atafakari amri mpya ya marufuku dhidi ya wahamiaji

Sekione Kitojo
13 Februari 2017

Rais Trump wa Marekani anatarajiwa kuwasilisha hatua mpya dhidi ya wahamiaji mapema leo Jumatatu(13.02.2017) kwa jina la kuiweka Marekani salama, mshauri wake akisisitiza rais hajakiuka mamlaka yake kwa marufuku hiyo.

https://p.dw.com/p/2XSKz
Trump signs an executive order at the White House in Washington
Rais Donald Trump wa Marekani akisaini moja kati ya amri za raisPicha: Reuters/K. Lamarque

Wakati  huu  ambapo  marufuku  hiyo  imezuiwa  na mahakama  kuu  ya  rufani  ikisubiri  mapitio  mengine  ya kisheria, Trump  "anatafakari  na  kuangalia  kila  njia," mshauri  wa  rais Stephen Miller  alikiambia  kituo  cha televisheni  cha  Fox News  jana  Jumapili.

Ikulu  ya  Marekani   inaweza ama  kufungua  rufaa  ya dharura  katika  mahakama  kuu, ikitetea  uzito wa  amri hiyo  katika  mahakama   za  chini  ama  kutoa  amri  mpya. Chaguo  la  mwisho  lilitolewa  na  Trump  binafsi  siku  ya Ijumaa.

Denver Trump Protest gegen Muslim Ban
Watu wakikusanyika katika uwanja mkuu wa jiji la Denver kwa maandamano wakiunga mkono jamii ya Waislamu.Picha: picture-alliance/AP Photo/B. Linsley

"Tunatafakari  hatua  mpya  na  za  ziada  kuhakikisha kwamba  uhamiaji  sio nyenzo  ya  kuwaruhusu  watu ambao  wanauhasama  na  taifa  hili  pamoja  na  maadili yake  kuingia  nchini," Miller  alisema  katika  kipindi  cha televisheni  ya  NBC kiitwacho "Kutana  na  wanahabari".

"Hakuna  kitu  kinachoitwa  ukuu  wa  mahakama. Kile ambacho  majaji  walifanya  ni  kuondoa  madaraka ambayo  yako  moja  kwa  moja  mikononi  mwa  rais  wa Marekani.

USA - New York Proteste für Planned Parenthood
Maandamano dhidi ya amri iliyosainiwa na rais Trump mjini New YorkPicha: picture-alliance/dpa/ZUMA WIRE/Pacific Press/E. Mcgregor

Mkutano na  waziri  mkuu wa  Canada

Suala  hilo  ni  hakika  kwamba  litajitokeza  wakati  rais Trump  atakapokutana  na  waziri  mkuu  wa  Canada Justin Trudeua  leo Jumatatu, ambaye  alisema  baada  ya rais  huyo  kutoka  chama  cha  Republican  kutoa  amri hiyo  ya  marufuku  kwamba  nchi  hiyo  jirani  ya  Marekani upande  wa  kaskazini  inawakaribisha  kwa  mikoni  miwili "wale  wanaokimbia  ukandamizaji , ugaidi  na  vita."

Kanada Weltweites Entsetzen nach Anschlag auf Moschee in Kanada Justin Trudeau
Waziri mkuu wa Canada Justin TrudeauPicha: picture alliance/empics/T. Korol

Wakati  hatima  ya  marufuku  ya  Trump  dhidi  ya wakimbizi  na  wasafiri  kutoka  mataifa  saba  yenye Waislamu  wengi  bado  inashikiliwa  na  mahakama, amri nyingine  ya  rais  inayotaka  kurejeshwa  makwao wahamiaji  ambao  hawana  hati  za  ukaazi  na hawajaorodheshwa  imesafisha  njia ya  kukamatwa  kwa mamia  ya  watu, wengi  wao  watu  kutoka  mataifa  ya Amerika  ya  kusini , wiki  iliyopita.

Wakati  maelfu  ya  Wamexico  waliandamana  jana  dhidi ya  kiapo  cha  Trump  kwamba  atailazimisha  nchi  hiyo kugharamia  ujenzi  wa  kile  alichosema "ukuta  mkubwa wa  kupendeza,"kati ya Marekani na Mexico, ikulu  ya Marekani  imethibitisha  mipango  ya  rais  kutafakari kuhusu  hatua  mpya  kuharakisha  kurejeshwa  makwao wahamiaji  haramu.

Katika  maandamano yaliyofanyika nchini  Mexico  kulaani  hatua  za  ukandamizaji  za  rais Trump kwa  wahamiaji  na  kutaka  kujenga  ukuta mwanasiasa  maarufu  wa  Mexico  Andres Manuel Lopez Abrador  alisema  hatua  ya  ujenzi  wa  ukuta  ni  kinyume na  ubinadamu.

Mexiko Anti Trump Demonstration
Maandamano dhidi ya Trump nchini MexicoPicha: Getty Images/AFP/R. Schemidt

"Wakitaka  kujenga  ukuta  kuwatenganisha  watu , ama wakati  neno "wageni" likitumika  kuwatukana, kuwadhalilisha  na  kwa  nia  ya  ubaguzi dhidi  ya binadamu  wenzetu, inakwenda  kinyume  na  ubinadamu, ni utovu wa  akili na  kinyume  na  historia."

Wakati  huo  huo Korea  ya  kaskazini  imesema  imefanya jaribio lililofanikiwa  leo  la  kombora, na  kuzusha  wito unaoongozwa  na  Marekani  kufanyika  haraka  kwa  kikao cha  baraza  la  Usalama  la  Umoja  wa  Mataifa baada  ya jaribio  hilo  kuonekana  kwamba  ni  changamoto  kwa  rais Donald Trump.

Muandishi: Sekione  Kitojo / afpe

Mhariri: Yusuf Saumu