1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump: Korea Kaskazini yapaswa kuwa na hofu

John Juma
11 Agosti 2017

Rais Trump azidisha vita vya maneno dhidi ya Korea Kaskazini kwa kusema kuwa labda kitisho cha awali alichokitoa dhidi ya Korea Kaskazini kuwa itakumbwa na moto mkubwa na ghadhabu nyingi hazikutosha.

https://p.dw.com/p/2i3pt
Nordkorea Raketentest Hwasong-14
Picha: Reuters/KCNA

Rais wa Marekani Donald Trump amezidisha vita vya maneno na vitisho kati yake na Korea Kaskazini kwa kusema kuwa labda kitisho cha awali alichokitoa dhidi ya Korea Kaskazini kuwa itakumbwa na moto mkubwa na ghadhabu nyingi hazikutosha. Wakati huo huo, baadhi ya nchi zimeanza kuelezea misimamo ya nchi ambazo zitaunga mkono vita vikitokea.

Rais Trump amesema Korea Kaskazini inapaswa kuwa na woga mwingi ikiwa itafanya chochote kwa Marekani. Kauli hii ya hivi karibuni kutoka kwa Trump inajiri baada ya vita vya maneno vya siku mbili kati ya Washington na Pyongyang, ikiwemo kitisho cha Korea Kaskazini kuwa itashambulia kisiwa cha Guam cha Marekani.

Seoul Donald Trump und  Kim Jong Un auf einem Screen
Picha: picture alliance/dpa/AP/A. Young-joon

Akizungumza kabla ya mkutano na washauri wa usalama wa Marekani akiwa jimbo la New Jersey, Trump amesema kuwa umewadia wakati wa mtu kusimama imara kwa raia wa Marekani na kwa nchi nyingine. "Hakika nadhani ni mara ya kwanza wamesikia kauli hiyo nilivyosema lakini  labda haikuwa thabiti sana. Wamekuwa wakifanya haya kwa nchi yetu kwa muda mrefu, miaka mingi na ni wakati wa mtu kujitokeza kwa raia wa nchi hii na wa nchi nyingine."

Australia kuisaidia Marekani

Kufuatia hofu ya uwezekano wa vita kutokea kati ya Marekani na Korea Kaskazini, hasa baada ya Pyongyang kutoa maelezo ya mipango yake kushambulia kisiwa cha Guam cha Marekani ambacho kinahifadhi kambi ya kijeshi ya Marekani, Waziri Mkuu wa Australia Malcolm Turnbull amesema kuwa nchi yake itajisaidia Marekani iwapo Korea Kaskazini itaishambulia Marekani kwani wao ni washirika wakuu na watatumia mkataba wa usalama wa ANZUS unaojumuisha Australia, New Zealand na Marekani.

Nordkorea Raketentest Hwasong-14
Picha: Getty Images/AFP/KCNA

Turnbull amesema "Mkataba wa ANZUS unamaanisha ikiwa Marekani imeshambuliwa, tutawasaidia. Ikiwa Australia imeshambuliwa, Wamarekani watatusaidia. umeunganishwa kwenye kiuno. Ushirikiano wa Marekani ni msingi wa usalama wetu."

Waziri wa ulinzi wa Japan naye amesema kuwa Tokyo haiwezi kukubali uchokozi kutoka kwa Pyongyang na kusema itatibua makombora ya Korea Kaskazini yatakayoelekezwa Marekani endapo yatatishia usalama wa Japan.

China yatoa masharti

Japo nchi hazijaunga mkono Korea Kaskazini, itapata usaidizi wa kimasharti kutoka kwa jirani yao China.

China imesema endapo Marekani itaishambulia Korea Kaskazini kwa lengo la kupindua serikali na kubadilisha mfumo wa kisiasa, basi China itawazuia kufanya hivyo. Hayo yamechapishwa kwenye gazeti linalomilikiwa na serikali la China,Global Times. Hata hivyo gazeti hilo halikupendekeza Beijing kuiunga mkono Pyongyang kwa namna yoyote ile

Mwandishi: John Juma/DPEA/AFPE

Mhariri: Mohammed Khelef