1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tuzo ya Nobel na hotuba ya rais wa shirikisho magazetini

Oumilkher Hamidou5 Oktoba 2010

Vitendo vifuate maneno wanasema wahariri waklichambua hotuba ya rais wa shirikisho mnamo siku ya kuadhimisha miaka 20 ya muungano

https://p.dw.com/p/PVfq
Mtoto wa kwanza kuzaliwa kutokana na uvumbuzi wa Robert EdwardsPicha: AP

Tuzo ya Tiba ya Nobel, mjadala kuhusu namna ya kujumuishwa waislam katika maisha ya kila siku ya jamii humu nchini na kitisho cha hujuma za kigaidi za wafuasi wa itikadi kali ya dini ya kiislam ni miongoni mwa mada zilizochambuliwa zaidi na wahariri wa magazeti ya Ujerumani hii leo.

Tunaanzia lakini na tuzo ya tiba ya Nobel.Gazeti la "Badische Zeitung" la mjini Freiburg linajiuliza kama aliyetunukiwa kweli amestahiki.Gazeti linaendelea kuandika:

Mambo yamekwenda vizuri na kumletea sifa na utukufu Robert Edwards pamoja pia na furaha kwa familia Brown.Lakini amestahiki kweli kutuzwa zawadi hiyo ya Nobel?Jibu ni ndio-amestahiki.Mtu aliyefanikiwa kuwapatia jaha mamilioni ya watu,hawezi kunyimwa tuzo kama hiyo.Lakini ukarimu mwengine mkubwa kama huo katika utafiti nyeti kama huo usiruhusiwe tena.Kwasababu ufanisi wa Edwards umefunguwa njia inayotisha.Tangu Louise Brown,watu hawahitaji tena kusubiri kwa hamu maumbile, wanadhibiti wenyewe mustakbal wao tena hata kabla ya kuzaa.

Gazeti la "Schwarzwälder Bote" linaandika:

Shauri muhimu la Edwards lilikuwa kuwasaidia binaadam.Na hilo amelitekeleza.Na ndio maana kamati ya Nobel imefanya vyema kwa kumteuwa muengereza huyo atunukiwe nishani hiyo muhimu kabisa ulimwenguni.Utafiti wa Edwards umewapatia jaha watu wengi.Kwa namna hiyo amegeuka kuwa baba wa kiroho wa mamilioni ya watoto kutoka kila pembe ya dunia.

Bundespräsident Christian Wulff Deutsche Einheit Rede
Rais wa shirikisho Christian Wulff akihutubia katika hafla ya kuadhimisha miaka 20 ya muungano wa UjerumaniPicha: picture alliance/dpa

Mjadala kuhusu juhudi za kujumuishwa wahamiaji katika maisha ya kila siku ya jamii yamepamba moto.Katika hotuba yake kuadhimisha miaka 20 ya kuungana upya Ujerumani,October tatu iliyopita,rais wa shirikisho alilizungumzia suala hilo pia.Gazeti la "Westdeutsche Zeitung" la mjini Düsseldorff linaandika:

Jinsi hotuba ya rais wa shirikisho Christian Wulff ilivyosifiwa inaonyesha matamshi yake yamegusia ndipo.Sasa vitendo vinabidi vifuate.Kwasababu maneno peke yake hayatoshi.Kwamba kazi haitokuwa rahisi,hali hiyo imeshuhudiwa wakati wa majadiliano tete kati ya serikali na jumuia za waislam.Hata hivyo hakuna njia nyengine isipokua hiyo.Ndio maana majadiliano yanabidi yaanze haraka ili wakati ambao ni tunu usipotee bure.

Mada yetu ya mwisho inahusu kitsho cha kutokea mashambulio ya kigaidi ya wafuasi wa itikadi kali ya dini ya kiislam.Gazeti la "Recklinghäuser Zeitung" linaandika:

Kinyume na watangulizi wake,Otto Schilly au Wolfgang Schäuble,waziri wa mambo ya ndani Thomas de Maizière hajitokezi kwa kishindo,badala yake anaangaliwa kama mlinzi mpole wa usalama wa ndani:hakuna kupalilia mambo,wala kutoa onyo, hii ni hali mpya inayojitokeza ikilinganishwa na zamani.

Gazeti la "Der neue Tag" la mjini Weiden linaandika:

Kinachotia wasi wasi ni kwamba onyo la kutokea mashambulio ya kigaidi limetokana na matamshi yaliyotolewa na wafuasi wa itikadi kali wa kijerumani wanaoshikiliwa katika jela ya Marekani huko Bagram nchini Afghanistan.Kituo hicho kinajulikana kama jela ya mateso ya CIA.Ikiwa matamshi hayo ni matokeo ya kuhojiwa vikali na kuteswa watuhumiwa hao,basi onyo hilo linastahili kuwekewa suala la kuuliza.Hata hivyo kimoja lazma kizingatiwe,kila onyo lazma lizingatiwe,kwa makoni na taratibu kama anavyofanya waziri wa mambo ya ndani Thomas de Maizière.

Mwandishi: Hamidou, Oumilkher/DPA/Inlandspresse

Mpitiaji: Josephat Charo