1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchaguzi mpya nchini Poland

Maja Dreyer13 Agosti 2007

Uchaguzi mpya nchini Poland ni suala linalozingatiwa katika magazeti mengi. Moja kwa moja basi tuanze na gazeti la “Berliner Zeitung” la uchambuzi wake juu ya hali ya siasa katika nchi hiyo kubwa jirani ya Ujerumani. Gazeti limeandika:

https://p.dw.com/p/CHSA

“Kwa muda wa mwaka mmoja, serikali hii imekumbwa na matatizo ya ndani. Wanasiasa wanalaumiana au vitendo vya udanganyifu vimegunduliwa. Hatimaye hata polisi imetumiwa katika mzozo kati ya vyama vilivyoingia katika serikali ya mseto. Hiyo siyo tena siasa ya kuaminika. Ndugu mapacha Kaczynski wanaotawala Poland mmoja akiwa waziri mkuu na mwingine rais walishindwa kutekeleza mageuzi ya maadili.”

Mhariri wa “Dresdner Neueste Nachrichten” anaangalia sifa ya serikali ya Poland na ameandika:

“Serikali ya Poland inatoa picha inayosikitisha baada ya mivutano ya ndani na sera mbaya. Imejiharibia yenyewe na pia iliathiri sifa ya nchi nzima. Baada ya waziri mkuu Jaroslaw Kaczynski alipoarifu kufanywa uchaguzi mpya, wananchi sasa wana matumaini mapya. Wanajua kuwa hali haitakuwa mbaya zaidi. Lakini je, hali kweli itakubwa bora baada ya uchaguzi? Kaczynski, kwa upande wake, anaamini atachaguliwa upya, kwani pale alipotangaza juu ya uchaguzi mpya, mara tu alianza kampeni yake. Iwapo siasa nchini Poland itabadilika itategemea nguvu ya upinzani ambao hauna muda wa kutosha kujiandaa na uchaguzi huu.”

Tunaendelea na suala la Iraq ambalo linazungumziwa na mhariri wa “Frankfurter Rundschau” akitegesha sikio juu ya jukumu la Marekani na Iran katika kuleta amani Iraq baada ya mazungumzo kati ya nchi hizo na ziara ya waziri mkuu al Maliki wa Iraq nchini Iran. Mhariri huyu ameandika:

“Hofu ya kuwa hali nchini Iraq inaweza kuporomoka zaidi inawatia wasiwasi majirani wote wa nchi hiyo ya vita. Hofu hiyo ni kubwa kuliko hata uadui mkali kati ya Iran na Marekani ambazo sana zinakaribiana kutafuta suluhisho, ila tu serikali za nchi zote mbili zinakanusha mabadiliko katika sera zake. Hata hivyo, ni habari muhimu sana, kwamba Iran na Marekani wanatafuta suluhisho la pamoja na inaonyesha kuwa nchi hizo zimefahamu haziwezi kutatua mzozo huu nchi moja peke yake. Marekani inapaswa kuisaidia Iraq katika kuimarisha serikali yake ambayo pia inakubali dai la Iran la kuwa na ushawishi wa kiwango fulani. Halafu, pande hizo tatu zishirikiane katika kupambana na wanamgambo badala ya kuchukua hatua dhidi ya mwingine kama wanavyofanya hadi sana.”

Kwa mwisho tena ni suala tofauti kutoka “Schwäbische Zeitung”. Gazeti hilo linakumbusha juu ya malengo ya Millenia na mahusiano yao na hali ya hewa duniani. Tunasoma:

“Malengo ya Millenia yaliyopitishwa na nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa mwaka 2000 yanataka umaskini duniani uwe nusu tu hadi mwaka wa 2015. Sasa nusu ya muda huu umepita, lakini matokeo hadi sasa ni madogo. Sababu kubwa ni mabadiliko ya hali ya hewa ambayo athari zake ni kwamba hali ni mbaya zaidi kuliko zamani katika maeneo mengi. Kwa muda mrefu mno wanasiasa walikanusha maonyo ya wanasayansi. Kwa hivyo tunashindwa kuamini tena kuwepo sera bora kwa ajili ya dunia bora. Lakini kupiga vita mabadiliko ya hali ya hewa ni sawa na sera za kuleta amani, kwani ugaidi na siasa kali zinaweza kukua vizuri pale ambako watu ni maskini."