1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchaguzi wa India waingia hatua muhimu

10 Aprili 2014

Wapiga kura nchini India leo wameingia katika siku muhimu kabisa katika uchaguzi mkuu wa nchi hiyo. Uchaguzi wa wabunge unafanyika katika majimbo muhimu, ukiwemo mji mkuu, New Delhi.

https://p.dw.com/p/1Bevv
Wananchi wa India wakipiga kura
Wananchi wa India wakipiga kuraPicha: Reuters

Uchaguzi wa leo ambao ni wa awamu ya tatu kati ya awamu tisa unafanyika kwenye majimbo 91 ya uchaguzi, yakiwakilisha karibu theluthi tano ya viti 543 vya bunge la India katika mji mkuu wa New Delhi na majimbo mengine 13, ikiwemo India Mashariki ambako wapiganaji wa Kimao wametishia kuuvuruga, huku chama cha kupambana na rushwa kikikabiliwa na mtihani mkubwa.

Hata hivyo, jicho linaelekezwa zaidi katika mji mkuu, New Delhi, ambako chama cha kupambana na rushwa cha Aam Aadmi-AAP kilianzishwa na kilichopata ushindi na kuchukua madaraka katika jimbo la Delhi mwezi Disemba mwaka uliopita.

Kiasi watu milioni 814 wa India wanatarajiwa kupiga kura katika uchaguzi huo ulioanza siku ya Jumatatu, ili kukiondoa madarakani chama tawala cha Hindu Nationalist kilichokuwa madarakani kwa miaka 10 na kumchagua mwanasiasa wa kihafidhina Narendra Modi wa chama cha BJP, wakati ambapo nchi hiyo inakabiliwa na ukuaji mdogo wa uchumi, rushwa pamoja na onyo kuhusu ghasia za kidini.

Kiongozi wa BJP, Narendra Modi
Kiongozi wa BJP, Narendra ModiPicha: uni

Chama hicho cha AAP kinagombania zaidi ya viti 400 vya bunge. Mbali na Delhi, uchaguzi huo pia unaangaliwa kwa karibu katika eneo la kaskazini mwa India ambako chama cha Bharatiya Janata-BJP, kinatarajiwa kupata ushindi mkubwa.

AAP chashiriki kwa mara ya kwanza

Chama cha AAP kinashiriki kwa mara ya kwanza katika uchaguzi mkuu, tangu kuanzishwa kwa chama cha kupambana na rushwa mwaka 2011, hatua iliyozusha hasira ya umma kutokana na kashfa kadhaa za rushwa. Chama hicho kimeahidi kujisafisha kisiasa kwa kuwaondoa wanasiasa wanaohusishwa na makosa ya uhalifu.

Kwa mujibu wa muungano wa mashirika ya mageuzi ya kidemokrasia-ADR, karibu asilimia kumi ya wanasiasa walioshiriki katika awamu ya kwanza ya uchaguzi huo siku ya Jumatatu, wamewahi kufunguliwa mashtaka ya jaribio la mauwaji, ubakaji pamoja na uhalifu mwingine.

Zoezi la kupiga kura likiendelea India
Zoezi la kupiga kura likiendelea IndiaPicha: Reuters

Mwezi uliopita, ADR, ilisema kuwa asilimia 37 ya wagombea wa chama cha BJP na asilimia 25 ya wagombea wa chama cha Congress cha AAP, waliotangazwa hadi sasa, wanakabiliwa na makosa ya uhalifu.

Chama cha AAP, kimesema kinatarajia kushinda viti 100 vya bunge na kwamba kina uhakika wa kushinda viti vitano kati ya viti saba vya bunge vinavyogombewa kwenye jimbo la Delhi.

Katika uchaguzi huo maeneo muhimu yanayoangaziwa zaidi ni pamoja na Kerala eneo la Kusini. Uchaguzi pia unafanyika katika jimbo la Kaskazini la Uttar Pradesh, ambalo litapeleka wajumbe 80 bungeni na lililokumbwa na ghasia za kidini mwezi Agosti mwaka uliopita. Matokeo ya uchaguzi huo ambao ni mkubwa kabisa kuwahi kushuhudiwa katika historia ya dunia, yanatarajiwa kutangazwa Mei 16.

Mwandishi: Grace Patricia Kabogo/AFPE
Mhariri: Josephat Charo