1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchaguzi wa wabunge nchini Urusi

Halima Nyanza30 Novemba 2007

Uchaguzi wa wabunge nchini Urusi unafanyika jumapili ya tarehe 2 baada ya kampeni kufungwa siku ya Ijumaa Novemba 30, huku chama cha Rais Putin kikiwa na uhakika wa ushindi mkubwa.

https://p.dw.com/p/CVH4
Rais Vladmir Putin ambaye chama chake kinatarajia kupata ushindi mkubwa.Picha: AP

Kampeni za uchaguzi huo zimemalizika jana siku ya Ijumaa huku chama cha United Russia kinachoongozwa na Rais Puttin kikitarajia ushindi wa kishindo.

Vyama kadhaa vya kisiasa nchini humo vimekuwa vikiwania nafasi kadhaa katika bunge la nchi hiyo yaani Duma.

Uchaguzi huo umekuwa ukifuatiliwa kwa karibu zaidi, hasa pia kutokana na kwamba awamu ya pili ya Rais Putin kukaa madarakani inamalizika mwakani, kwa mujibu wa katiba ya nchi hiyo Rais Putin haruhusiwi tena kugombea.

Katika siku za mwisho za kampeni za chama chake Rais Putin alinadi wabunge wa chama chake kwa kutoa maelezo mbalimbali kuhusu nini walichofanya wakati wa uongozi wao hususan katika kuinua uchumi wa nchi hiyo na pamoja na kuondoa umasikini.

Putin anaelezea zaidi,

‚’Tarehe mbili ya mwezi Desemba mwaka huu, kutafanyika uchaguzi wa wabunge kitaifa, na mpaka sasa katika kampeni za uchaguzi kumeshatolewa ahadi mbalimbali na wagombea, lakini sasa napenda kuzungumzia hili, tumefanya kazi kubwa japokuwa hatukufanikisha yote kwani kazi ilikuwa ngumu, hakuna kitu kisichokuwa na makosa..Tumejitahidi kuinua uchumi wa nchi, kupambana na umasikini, rushwa, ugaidi….

Na pia nataka mlizingatie hili ushindi wa wabunge wa chama changu ni ushindi kwa raisa mpya ajae’’.

Awali Rais Puttin aliwalaumu wapinzani wake kwa kutaka kuvuruga uchaguzi huo, na akidai zaidi kuwa wanatafuta kuungwa mkono na nchi za magharibi, kutokana na wapinzani hao kutoa lawama mbalimbali za upendeleo unaopewa chama chake katika kipindi chote cha kampeni.

Serikali ya Urusi ilikana na kusema kuwa uchaguzi utakuwa wa haki

Katika hatua nyingine Jumuia ya Ulaya inayoshughulikia masuala ya Usalama na Ushirikiano ilitishia kujitoa kama mwangalizi wa kimataifa katika uchaguzi huo baada ya Urusi kukawia kutoa pasi ya kuingilia nchini humo.

Rais Putin pia aliilaumu Marekani na Jumuia hiyo ya Ulaya ikwamba zimedhamiria kuufedhehesha uchaguzi huo wa duma unaotarajia kufanyika kesho.

Hata hivyo Marekani ilipinga suala hilo na kuitaka Urusi kuthibitisha hilo.

Rais PUTIN atamaliza kipindi chake cha kuongoza nchi hiyo baada ya uchaguzi mwakani lakini wachunguzi wa mambo wanasema kuwa uongozi wa kremlin unataka kuendelea kuwa kama ulivyo hata baada ya Rais Putin kuondoka madarakani, lakini hiyo yote itategemea na matokeo ya uchaguzi wa wabunge katika bunge la nchi hiyo yaani Duma.

Wagombea wa nafasi ya kiti cha Urais nchini Urusi katika uchaguzi unaotarajia kufanyika mwezi Machi mwaka ujao wanatakiwa kujiandikisha Decemba 23 mwaka huu, kwa sasa serikali iliyopo madarakani ipo katika kazi nzito ya kutangaza mgombea wake.