1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchambuzi kutoka magazeti ya Ujerumani ya leo asubuhi

1 Novemba 2007

Miaka mitatu na nusu baada ya mashambulio ya kigaidi dhidi ya wakaazi wengi wa mjini Madrid, Spain, ile kesi dhidi ya washtakiwa 28 wa tokeo hilo imemalizika kwa kutolewa hukumu. Katika magazeti ya Ujerumani kumetawala hali ya kuridhika na mfumo wa sheria wa Spain

https://p.dw.com/p/C7l4

Gazeti la FRANKFURTER ALLGEMEINE ZEITUNG liliandika hivi:

+Spain ni nchi ya kwanza ya magharibi ambayo, kufuatana na sheria na kanuni, imeweza kukamilisha kesi dhidi ya ugaidi wa itikadi kali za Kiislamu. Kile ambacho hakijawezekana kufanyika hadi sasa, baada ya mashambulio ya Septemba 11 huko Marekani au yale ya July 25 mwaka 2005 huko Uengereza, sasa kimeweza kufanywa na mahakama ya Spain. Kutokana na ushahidi ulio imara wamepatikana na hatia watu wenye siasa za kichwa ngumu wa kikundi, wengi wao wa kutokea Moroko, pamoja na wasaidizi wao wa huko huko Spain.+

Pia gazeti la LÜBECKER Nachrichten limeridhika na hukumu iliotolewa jana huko Madrid:

+Haijawa rahisi kwa mahakama ya Spain kuendesha kesi hii inayohusu shambulio baya kabisa la kigaidi nchini humo. Lakini mahakama imefanya ndivyo, kwani iliweka uwazi ulio mkubwa kabisa. Sehemu kubwa ya kesi hiyo ilionyeshwa kupitia televisheni au kutangazwa katika Internet. Na yote yaliosemwa mahakamani yanapatikana katika kanda za DVD. Mtindo huu wa kuendesha kesi katika Spain hautoi, lakini, dhamana kwamba hakutatokea mashambulio zaidi ya kigaidi, lakini ulikumbusha kwanini kunaendeshwa mapambano dhidi ya ugaidi. Heko kwa Spain.+

Gazeti la WESDEUTSCHE ZEITUNG pia linaona kuna athari nzuri kutokana na kesi hiyo:

+ Kufanyiwa kazi, kisheria, mashambulio ya kigaidi ya Madrid ya Machi 11, 2004 kumeweka katika mwangaza mambo mengi yalio machungu. Masomo hayo yaliopatikana kutoka asubuhi hiyo kwenye mji mkuu wa Spain haitoweza kuwasaidia zaidi watu 191 waliokufa katika mkasa huo, hata ikiwa sasa magaidi wamehukumiwa adhabu kubwa na mahakama na watapelkwa gerezani. Ukweli huu tutarajie utakuwa ni mchango wa kuzuwia mashambulio mepya ya kigaidi.+