1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchunguzi wa madai ya njama ya Trump na Urusi wakosolewa

Bruce Amani
16 Mei 2023

Uchunguzi wa shirika la upelelezi la Marekani – FBI kuhusu madai ya kuweko njama kati ya Urusi na kampeni ya urais ya Donald Trump mwaka wa 2016 haukuwa na ushahidi halisi.

https://p.dw.com/p/4RRwr
USA Donald Trump
Picha: Evan Vucci/AP Photo/picture alliance

Mwanasheria huyo aliyeteuliwa na serikali miaka minne iliyopita amebaini uchunguzi huo wa FBI pia ulikuwa na dosari nyingi. 

Ripoti hiyo ya karibu kurasa 300 inahitimisha uchunguzi wa miaka minne ulioanzishwa Mei 2019. Aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa wakati huo William Barr alimteuwa Durham, mwendesha mashitaka mkongwe, kuchunguza uwezekano wa dosari zilizofanywa na FBI.

Kwa wakati huo, FBI ilikuwa tu ndio imeanzisha uchunguzi mkali kuhusu uwezekano wa mawasiliano kati ya timu ya kampeini ya Donald Trump ya urais wa 2016 na Urusi. Uchunguzi huo kisha baadae ukakabidhiwa mwanasheria maalum Robert Mueller, ambaye Machi 2019 alihitimisha kuwa hakukuwa na ushahidi wa njama ya uhalifu kati ya kampeni ya Trump ya 2016 na Urusi.

FBI chini ya ukosoaji mkali

Bolton amzamisha Trump

Durham amekosoa vikali vyanzo vya uchunguzi wa FBI. Ripoti yake imesema si maafisa wanaosimamia utekelezaji wa sheria Marekani wala jamii ya ujasusi wanaoonekana kuwa na ushahidi wowote halisi wa kuwepo njama kati ya Urusi na kampeni ya Trump ya mnamo mwaka 2016 wakati walipoanzisha uchunguzi wao.

Katika jibu lake kwa ripoti hiyo, FBI imesema tayari imetekeleza hatua kadhaa za kurekebisha kasoro ambazo zimekuwepo kwa muda sasa.

Durham aelezea FBI undumilakuwili

Durham, mwendesha mashtaka wa zamani wa serikali, amesema FBI na Wizara ya Sheria walionyesha undumilakuwili katika namna ambavyo walimchunguza Trump ikilinganishwa na mpinzani wake wa uchaguzi wa kuingia White House 2016, Mdemocrat Hillary Clinton.

Ripoti hiyo imesema kasi na namna ambavyo FBI walianzisha uchunguzi uliopewa jina la siri la Crossfire Hurricane wakati wa msimu wa uchaguzi wa rais kutokana na taarifa za kijasusi ambazo hazijapitiwa, kuchambuliwa, na kuthibitishwa pia kulionyesha tofauti na jinsi walivyoyashughulikia masuala ya hapo kabla yaliyohusisha uwezekano wa jaribio la mipango ya uingiliaji wa kigeni katika uchaguzi uliolenga kampeni za Clinton.

Trump aikaribisha ripoti

Trump, ambaye anawania uteuzi wa chama cha Repiblican kuelekea uchaguzi wa rais, ameikaribisha ripoti hiyo ya Durham. Ameandika ujumbe kwenye mtandao wake wa kijamii wa Truth Social kuwa Mwanasheria maalum Durham amehitimisha kuwa FBI haikupaswa hata kuanzisha uchunguzi kuhusu njama ya Trump na Urusi.

Kwa maneno mengine, umma wa Marekani ulilaghaiwa, kama unavyofanyiwa hadaa hivi sasa na wale ambao hawataki kuuona ubora wa Marekani, akionekana kumaanisha uchunguzi unaoendelea wa kesi kadhaa za uhalifu dhidi yake.

Vyanzo