1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uhispania kuitawala Catalonia moja kwa moja

27 Oktoba 2017

Waziri Mkuu Uhispania amelihutubia bunge Ijumaa kabla kura itakayoamua kutolewa mamlaka ya kikatiba, yatakayoidhinisha kuchukuliwa kwa mamlaka ya jimbo la Catalonia, katika harakati za kusitisha eneo hilo kupata uhuru.

https://p.dw.com/p/2mbsx
Spanien Ministerpräsident Mariano Rajoy leitet eine Kabinettssitzung zur Durchsetzung des Artikels 155
Waziri Mkuu wa Uhispania Mariano RajoyPicha: picture-alliance/AP Photo/J. C. Hidalgo

Mariano Rajoy, amesema hatua ya kwanza ya serikali itakuwa kumuondoa rais wa jimbo hilo Carles Puigdemont iwapo atapewa mamlaka maalum na bunge la seneti la nchi hiyo.

Rajoy amesema iwapo hatua hizo zitaidhinishwa, serikali ya Uhispania itamuachisha kazi rais wa Catalonia Carles Puigdemont na mawaziri wake. Kiongozi huyo wa Uhispania amesema, kinachotokea Catalonia ni ukiukaji wa wazi wa sheria, demokrasia na haki za kila mmoja na kwamba jambo hilo lina adhabu yake. Ameongeza kwamba, hatua hizo ndizo zitakazositisha mzozo huo.

Rajoy vile vile ameliambia baraza la seneti, kuwa rais wa Catalonia alikuwa na nafasi ya kusitisha kuenea kwa mzozo huo ila alikataa kufanya hivyo, "yeye ndiye wa kulaumiwa kwa kuidhinishwa kwa matumizi ya kile kipengee 155 cha katiba," alisema Rajoy.

Kuna wasiwasi kuhusiana na jinsi serikali kuu itakavyotawala

Kipengele hicho cha 155 cha katiba ya Uhispania  kinairuhusu serikali kuu kuchukua utawala wa eneo iwapo litavunja sheria.

Spanien Demonstration für Unabhängigkeit Katalonien in Barcelona
Wakaazi wa Catalonia wakitaka uhuru waoPicha: Getty Images/S. Gallup

Hatua hiyo ya Uhispania ya kutaka kuiongoza Catalonia moja kwa moja huenda ikazusha hali ya wasiwasi, ukizingatia kwamba bunge la Catalonia nalo litafanya kikao maalum leo ambapo tangazo rasmi la uhuru huenda likatolewa.

Vile vile kuna hali ya wasiwasi kuhusiana na jinsi serikali kuu itakavyonyosha mkono wake wa kutawala huko Catalonia na iwapo Wacatalonia wenyewe watakubali. Elisabeth mwenye umri wa miaka 42, ni mkaazi wa Catalonia.

"Kusema kweli, sijui, natumai mambo yatakuwa mazuri kwetu," alisema Elisabeth, "natumai watatuangalia na huko Madrid wafahamu kwamba kuna tatizo kubwa hapa na haliwezi kusuluhishwa na yale wanayofanya kwa sasa," aliongeza mkaazi huyo wa Barcelona.

Rajoy ataliita baraza lake la mawaziri baada ya kura ya seneti

Idhini ya Seneti ambapo chama cha Waziri Mkuu Rajoy kinajivunia idadi kubwa ya wabunge, ni hatua muhimu kwa serikali kuu kuanzisha utawala wa moja kwa moja huko Catalonia. Kura katika bunge hilo inatarajiwa kupigwa baadae hii leo.

Spanien Katalonien Carles Puigdemont Rede in Barcelona
Rais wa Catalonia Carles PuigdemontPicha: Reuters/Y. Herman

Baada ya hapo Rajoy anatarajiwa kuliita baraza lake la mawaziri kutekeleza hatua za kwanza za kuiongoza Catalonia moja kwa moja kutoka Madrid.

Hapo Alhamis rais wa Catalonia Carles Puigdemont aliamua kutoita uchaguzi wa bunge la eneo hilo, njia inayodhaniwa kuwa ndiyo ya pekee ya kuhakikisha kuwa serikali kuu kutoka Madrid haichukui mamlaka ya serikali yake. Puigdemont ameonya kuwa hatua ya serikali kuu kuchukua mamlaka yake ni jambo ambalo huenda likauchochea zaidi mzozo huo.

Mwandishi: Jacob Safari/AFPE/APE/DPAE/Reuters

Mhariri: Gakuba Daniel