1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uingereza yaamua kujitoa katika EU

Admin.WagnerD24 Juni 2016

Wananchi wa Uingereza wamepiga kura ya maoni iwapo nchi ibakie au ijiondoe kwenye Umoja wa Ulaya. Mchuano ulikuwa mkali matokeo yanaonyesha Brexit yashinda.

https://p.dw.com/p/1JCEC
Großbritannien EU-Referendum Brexit Nigel Farage
Nigel Farage mkuu wa chama cha UK Independence akifurahia ushindi katika matokeo ya awaliPicha: Reuters/T. Melville

Wananchi wa Uingereza wamepiga kura ya maoni jana(23.06.2016) iwapo wabakie katika Umoja wa Ulaya ama la na kura hiyo ya maoni imefanyika katika mazingira ya ongezeko la shakashaka kuhusu Umoja huo katika mataifa mengi ya kundi hilo, na ni moja kati ya kura kadhaa za maoni kuhusu Umoja huo.

Kura za maoni za kitaifa katika muda wa miaka 44 iliyopita imeweza kuelekeza mara nyingi mwelekeo uliochukuliwa na Umoja wa Ulaya , iwapo ni kwa kuwaingiza wanachama wapya, kupanua madaraka yake kupitia mabadiliko ya mikataba, ama kuingia katika miradi mipya.

Großbritannien EU-Referendum Brexit Wahlergebnis
Waungaji mkono wa kujitoa katika Umoja wa Ulaya wakishangiria matokeoPicha: picture alliance/empics/S. Rousseau

Wanorway walipiga kura kuwa nje ya jumuiya hiyo ya kiuchumi Septemba 1972 na tena Novemba 1994 wakati Austria , Finland na Sweden zilipojiunga na kile ambacho kimekuwa tangu wakati huo Umoja wa Ulaya.

Uingereza haijafanya kura ya maoni juu ya iwapo kujiunga na EEC , Jumuiya ya kiuchumi ya Ulaya mwaka 1973, lakini serikali iliyokuwa madarakani ya chama cha Labour iliyokuwa chini ya waziri mkuu Harold Wilson , ilitayarisha kura mwaka 1975 ambapo wapiga kura waliamua kubakia kwa asilimia 67.2.

Mkataba wa Maastricht , ukiweka msingi wa kuundwa kwa Umoja wa Ulaya na umoja wa sarafu ya Umoja huo, haikwenda kwa ulaini.

Hapo Juni 2, 1992 , raia wa Denmark waliwashangaza majirani zao wa Ulaya wakati walipokataa mkataba huo kwa asilimia 50.7.

Großbritannien EU-Referendum Brexit Auszählung der Stimmen in Manchester
Mabunda ya karatasi za kupigia kura yanawekwa katika kituo cha kuhesabiaPicha: picture alliance/AP Photo/D. Lawson

Waliunga mkono waraka uliofanyiwa mabadiliko kwa wingi mdogo Mei mwaka 1993, lakini ni baada ya Denmark kupata uhuru mkubwa wa kujitawala katika masuala ya ulinzi, sarafu, uraia na ushirikiano katika masuala ya sheria.

Wingi mdogo wa wapiga kura wa Ufaransa , asilimia 51.05 , uliidhinisha mkataba huo katika kura ya maoni iliyofanyika Septemba 20,1992.

Sarafu ya euro

Nchi mbili zilifanya kura ya maoni ya kujiunga na sarafu ya euro, ambayo iliundwa mwaka 1999.

Mwezi Septemba 2000 , kiasi kidogo juu ya asilimia 53 ya Wadenmark walikataa sarafu ya pamoja, na mwezi Septemba mwaka 2003, nchi jirani ya Sweden iligundua kwamba asilimia 56.1 ya wapiga kura wanataka sarafu yao ya krona.

Großbritannien EU-Referendum Brexit Wahlergebnis Sunderland
waungaji mkono wa upande wa kubakia wakiangalia matokeoPicha: Reuters/R. Stothard

Walipoulizwa kuidhinisha katiba ya Umoja wa Ulaya Mei mwaka 2005 , karibu asilimia 55 ya wapiga kura wa Ufaransa walisema , "Hapana" na zaidi ya asilimia 61 ya Waholanzi walikataa mswada huo wa katiba siku tatu baadaye.

Mkataba wa Nice ulikuwa na mabadiliko muhimu ya katiba yanayohitajika katika kupanua kundi hilo la mataifa upande wa mashariki mwaka 2004.

Mabadiliko hayo ya katiba yalikumbana na kura ya maoni nchini Ireland ambako awali yalikataliwa kwa asilimia 54 mwezi Juni 2001 wakati waungaji mkono waliudharau upinzani nchini humo.

Baada ya kupata garantii kuhusiana na kile kinachoenziwa sana na Waireland kuhusiana na kuwapo kati kwa kati kati masuala ya kijeshi, kura ya pili ya maoni iliidhinisha kwa asilimia 62.9 Oktoba 19, 2002.

Großbritannien EU-Referendum Brexit Wahlergebnis Sunderland
Watu wakifurahia matokeo ya kura ya maoni nchini UingerezaPicha: Getty Images/J. Taylor

Mkataba wa Lisbon

Ilikuwa hali hiyo hiyo kuhusiana na mkataba wa Lisbon, uliojadiliwa kuchukua nafasi kwa sehemu fulani ya katiba ya Umoja wa Ulaya . Juni 12, 2008 Ireland ilisema , "hapana" , lakini iliuidhinisha baada ya kufanyika kura ya pili ya maoni Oktoba 2009.

Mapema mwezi wa Aprili asilimia 61 ya Waholanzi walikataa mkataba muhimu wa Ulaya na Ukraine katika kura ya maoni isiyolazimisha inayoonekana kama kipimo cha hisia za kupinga Umoja wa Ulaya.

Zoezi la kuhesabu kura katika kura ya maoni nchini Uingereza linaendelea na kwa sasa ni matokeo ya majimbo 304 kati ya majimbo 382 yaliyopatikana , ambapo kambi ya kuondoka inaongoza kwa asilimia 51.72 dhidi ya 48.28 ya kubakia. Safari hata hivyo inaelekea kuwa ngumu kwa kambi ya kubakia na matokeo yanaonesha kwamba upande wa kujitoa unaweza kushinda .

Mwandishi: Sekione Kitojo..... / rtre / dpae