1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uingereza yaionya Libya kutosherehekea mwaka mmoja tokea kuachiwa Megrahi

Aboubakary Jumaa Liongo20 Agosti 2010

Leo ni mwaka mmojka tokea kuachiwa huru kwa mhusika wa shambulio la bomu dhidi ya ndege ya abiria ya Marekani katika anga la Lockerbie, Abdelbaset Ali Mohammed al-Megrahi ,

https://p.dw.com/p/OsSX
Abdel Baset al-Megrahi, mwenye suti nyeusi aliporeja Libya mwaka jana akiwa na kiongozi wa Libya Seif al-Islam Gadhafi kuliaPicha: AP

Uingereza  imeionya  Libya  kuwa  sherehe  zozote  za  kuadhimisha  siku hiyo, zitakuwa ,  ni  kinyaa ,  zinazoonyesha   dharau  na  kutokuwa  na  hisia.

Wizara  ya  mambo  ya  kigeni  ya Uingereza imetoa  wito  wa  kujizuwia  huku kukiwa  na  hofu  kuwa  inawezekana  kutokea  hali  kama   iliyotokea  mwaka jana  wakati  Abdelbaset  Ali  Mohammed  al-Megrahi  aliporejea  nyumbani na  kupokewa  kama  shujaa  nchini  Libya   baada  ya  kuachwa  huru.

Serikali  ya  Scotland , ambayo  ndiyo  iliyochukua  uamuzi  wa  kumuachia huru  mshambuliaji  huyo  kutoka  Libya , pia  inaripotiwa  kuitaka   Libya kujiepusha   kufanya  sherehe  mwaka  huu, ikisema  kuwa   matukio  yoyote ya   hadhara   yatakayofanyika  kwa  heshima  ya  Megrahi  yatalaaniwa.

Serikali  ya  Scotland  iliyokabidhiwa  mfungwa  huyo  ilimwachia  huru  kwa misingi  ya  kumuonea  huruma  hapo  August  20  mwaka  jana, ikisema kuwa   ni  mgonjwa  sana  akiwa  na   saratani  ya  tezi  za  kibofu  na  huenda ana  weza  kuishi  kwa  muda  wa  miezi  mitatu tu.

Lakini  Megrahi  bado  yu  hai  hadi  leo  nchini  mwake, na  kuzusha  hasira miongoni  mwa  ndugu  wengi  wa  watu  270  ambao  wameuwawa  wakati ndege  ya  shirika  la  ndege  la  Marekani, Pan Am  ilipolipuka  katika  anga ya  Lockerbie  nchini  Scotland Desemba  mwaka  1988.

Wakala  huyo  wa  zamani  wa  ujasusi , mwenye  umri  wa  miaka  58, alikuwa mtu  pekee  aliyehukumiwa  kuhusiana  na  uovu  huo , na  aliachiliwa  baada ya  kutumikia  kifungo  cha  miaka  minane  kati  ya  miaka  20  aliyohukumiwa.

Kuachiwa  kwake  kumeleta  mtikisiko  katika  uhusiano  baina  ya  Marekani Uingereza na  hata  baina  ya  serikali  za  Scotland  na   Uingereza. Scotland imekuwa  ikitetea  uamuzi  huo,  wakati  Uingereza  ikisisitiza   kuwa  inaamini uamuzi  huo  ulikuwa  ni  makosa.

Msemaji  wa   wizara  ya  mambo  ya  kigeni  mjini  London  jioni  ya  Alhamis ameitaka  Libya   kutofanya  sherehe  kwa  heshima  ya  mtu , aliyehukumiwa kwa  kufanya  tukio  baya  la  kigaidi  katika  historia  ya  Uingereza.

Hususan  katika  siku  ya  leo  ya  maadhimisho  tunatambua  maumivu makali  yanayoendelea  ambayo  yamesababishwa  kwa  wahanga,  kutokana na  kuachiliwa  huru  kwa  Megrahi, nchini  Uingereza  na  Marekani , msemaji huyo  amesema.

Sherehe  zozote  za  kuachiwa  kwa  Megrahi  zitakuwa  ni  kinyaa, zinazoonesha  dharau  na  zinazoonesha  kutokuwa  na  hisia  kwa   familia  za wahanga.

Ameongeza  kuwa  tumeweka  wazi  wasi  wasi  wetu  kwa  serikali  ya  Libya. Balozi  wa  Uingereza  nchini  Libya, Richard Northern, ameweka  wazi kwa maafisa  waandamizi  wa  serikali  ya  Libya  kuwa  tukio  lolote  la   hadhara kwa  heshima  ya  Megrahi linaweza  kuharibu  uhusiano baina  ya  nchi  hizo mbili, limeripoti  gazeti  la  Guardian  nchini  Uingereza.

Waziri  wa  sheria  wa  Scotland Kenny MacAskill, ambaye  alichukua  uamuzi huo  kumuachia  huru  al-Megrahi, ametetea  hatua  hiyo  jana , akisema , ulikuwa  ni  uamuzi  ambao  alipaswa  kuuchukua.

Mwandishi : Sekione Kitojo /AFPE

Mhariri: Aboubakary Liongo