1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

070610 Sparpaket Entwicklungshilfe

Abdu Said Mtullya8 Juni 2010

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel amesema misaada ya maendeleo itaendelea kutolewa.

https://p.dw.com/p/Nkeh
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel.Picha: AP

Serikali ya Ujerumani pia imepitisha mpango wa kubana matumizi kwa lengo la kukabiliana na nakisi kubwa katika bajeti yake.

Ujerumani itapunguza matumizi kwa kiasi cha Euro Bilioni 10 kila mwaka hadi mwaka 2016.
Lakini habari za kufurahisha ni kwamba misaada ya maendeleo kwa ajili ya nchi masikini haitapunguzwa.

Licha ya kupitisha mpango huo serikali ya Ujerumani imesema misaada ya maendeleo kwa ajili ya nchi masikini haitaguswa.Hayo ameahidi Kansela wa Ujerumani Angela Merkel baada ya kikao cha siku mbili na baraza lake la mawaziri mjini Berlin.Pamoja na hayo Kansela Merkel amehakikisha kwamba nchi yake itaendelea kulenga shabaha ya kuongeza msaada huo hadi asilimia 0.7 ya pato lake la taifa kwa ajili ya kuzisaidia nchi masikini hadi kufikia mwaka wa 2015. Kansela Merkel amesema Ujerumani itaendelea kulenga shabaha hiyo kwa uthabiti.Lakini amesema wazi kwamba lengo hilo siyo jukumu rahisi.

Waziri wa ushirikiano wa maendeleo wa Ujerumani Dirk Niebel ametaka kuongezwa kwa bajeti ya wizara yake kwa kiasi cha Euro milioni mia nne lakini hayo hayakuwezekana.Lakini serikali ya Ujerumani itatenga fedha zaidi kwa ajili ya elimu na utafiti katika mwaka ujao kuliko zinazotolewa mnamo mwaka huu.

Lakini katibu wa maendeleo Hans -Jürgen Beerfeltz amesema licha ya hali ngumu, misaada kwa ajili ya maendeleo bado inaungwa mkono na wananchi.Amesema wakati wote ni theluthi 2 ya wananchi wa Ujerumani wanaosema ,licha ya mgogoro, serikali ya Ujerumani inapaswa kutekeleza wajibu wake wa kimataifa katika suala la misaada ya maendeleo sambamba na kuendeleza harakati za kupambana na umasikini duniani.Ujerumani kwa sasa ina bajeti ya Euro Bilioni 6.7 kwa ajili ya misaada ya maendeleo.

Mwandishi/Bernd Gräßler/ZAR

Tafsiri/Mtullya Abdu.

Mhariri/Abdul-Rahman