1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani kuwa na waangalizi wa uchaguzi kwa mara ya kwanza

Thelma Mwadzaya27 Septemba 2009

Uchaguzi wa bunge nchini Ujerumani unafanyika leo na kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi hii, kutakuwa na waangalizi wasioegemea upande wowote kutoka katika Jumuiya ya usalam na ushirikiano wa kiuchumi (OSCE).

https://p.dw.com/p/Jq2J
Kansela Angela Merkel na mumewe Joachim Sauer wakipiga kuraPicha: AP

Nchi 56 za Ulaya na Amerika ya Kaskazini ni wanachama wa Jumuiya hiyo na Ujerumani ni moja kati ya wachangiaji wakubwa. Hata hivyo kwa kaßlt;waida mpango wa OSCE katika kusimamia chaguzi unalenga kwa ukaribu zaidi katika nchi ambazo hali zake za demokrasia ni za shakashaka.

Hatua hii ya kuwepo waangalizi katika uchaguzi huu imesababisha baadhi ya watu nchini Ujerumani kupendekeza kuwa, mpango huo hauna umuhimu wowote, na wengine wakisema kuwa hatua hiyo inashusha hadhi, na kwamba Ujerumani haihitaji uangalizi wa aina hiyo.

Lakini kwa waangalizi wenyewe hali ni tofauti. Wanaona kazi hiyo ni ya kitaalamu na shauku kubwa kama zilivyo kazi nyinginezo.

Symbolbild Wahlen Wählen Wahl Bundestagswahl
Karatasi ya kupigia kuraPicha: dpa

Kuna maafisa wa usimamizi ambao wamekuwa wakisubiri kupata fursa ya kusimamia uchaguzi nchini Ujerumani, tangu mwaka mmoja uliopita, wakiomba OSCE iandae mpango wa usimamizi wa uchaguzi nchini Ujerumani.

Elena Gnedna ni mmoja wa waangalizi hao wa uchaguzi na ni mwanafunzi anayefanya shahada yake ya udaktari katika sayansi ya siasa akitokea nchini Russia, ni mara yake ya kwanza kufanya kazi na OSCE, na ana shauku kubwa"Nimezaliwa Urusi, na baada ya kumaliza shule kulikuwa na miaka migumu sana ya mabadiliko ya kisiasa, hivyo nikajiuliza Urusi imekuwa nchi ya kidemokrasia au hapana, nikavutiwa na siasa, na nikaja kusoma ulaya, nikawa nimevutiwa na siasa kwa miaka yote. Na sasa nipo hapa. Lakini nina shauku zaidi na nchi za Ukraine na Moldova na zile Jamhuri za kisovieti ya zamani, ambazo bado yamo katika kipindi cha mabadiliko ya kidemokrasia."

Tathmini ya mfumo

Maamuzi kwa upande wa umma hushawishiwa zaidi na maslahi ya vyombo vya habari . Lakini maswali yanayoulizwa sio jambo ambalo mtu angelitarajia. Mpango huu wa kutathmini uchaguzi, unajikita zaidi katika kuingilia mfumo wa uchaguzi wa Ujerumani, kuliko suala lenyewe la upigaji kura.

OSCE yenyewe pamoja na umma wa wajerumani, wana imani kuwa zoezi la kuhesabu kura litakuwa la wazi, kwa hivyo mpango wa usimamizi utazingatia zaidi mfumo wa uchaguzi, kampeni na masuala kama uandikishaji wa wapiga kura yanavyoshugulikiwa.

Armin Ribitsch ni mtaalamu wa sayansi ya siasa kutoka Austria, ambaye anasema katika kipindi cha miaka minne au mitano ameshiriki katika zoezi la usimamizi wa uchaguzi sehemu mbalimbali duniani, zaidi ikiwa barani Afrika, lakini pia katika nchi kama Fiji, Yemen, Lebanon na Palestina. Yeye anasema,"Nafikiri hakuna mfumo wa uchaguzi ambao ni kamilifu, kwa hiyo mara zote tunaposhiriki katika usimamizi huwa tunakuja na mapendekezo, kwa hiyo hata hapa inaweza ikatokea hitilafu wakati wa mchakato wa uchaguzi, tutajaribu kutengeneza ripoti ambayo itatumika kwa wadau wa uchaguzi katika nchi husika ili kuboresha mfumo wa kazi kwa chaguzi za baadaye."

Kura mbili

Mfumo wa uchaguzi wa ujerumani ni tofauti. Mpiga kura anapokwenda katika kituo cha kupigia kura, huwa anapiga kura mbili. Kwanza humpigia mtu anayetetea kiti hicho moja kwa moja, na kura ya pili inatumika kwa ajili ya chama chake.

Huu ni mfano mzuri wa kitu ambacho OSCE inakichunguza. Chaguzi za Ujerumani huchukuliwa kama huru na za kiungwana, lakini mfumo wake ni mgumu.

Mwandishi: Lazaro Matalange

Mhariri: Abdul-Rahman