1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani na Norway uwanjani leo

25 Septemba 2007

Nusu-finali 2 za kombe la dunia la wanawake nchini China ni kati ya Ujerumani na Norway leo na Brazil na Marekani.Timu gani 2 zitakutana katika finali ni vigumu kuagua.

https://p.dw.com/p/CHay
Mshabiki huyu wa Kichina anasubiri kwa hamu fainali
Mshabiki huyu wa Kichina anasubiri kwa hamu fainaliPicha: dpa - Bildfunk

Timu ya wasichana wa Ujerumani katika kombe la dunia la wanawake nchini China, imepania leo kuichezesha Norway kindumbwe-ndumbwe katika nusu-finali ya kombe hilo.

Ujerumani, mabingwa watetezi walianza kwa mshindo mkubwa walipojaza kikapu cha Argentina mabao 11.

Juzi wakatamba na kuitimua Korea ya kaskazini mabao 3:0 na sasa wanadai hakuna timu ya wasichana ya wakuwazuwia kuingia finali kutetea taji lao.

Baada ya kuirarua Argentina kwa mabao 11:0,wajerumani walizimwa kasi yao na waingereza walipoachana 0:0.Baadae wakaitimua japan kwa mabao 2:0 na kuparamia kileleni mwa kundi A.

Sasa wasichana wa Ujerumani wakiwa mechi 2 kabla kurudi na kombe Ujerumani kwa mara ya pili mfululizo,wanarudi uwanjani leo bila hata kushindwa mara moja katika kombe hili na hata bila ya kukomewa bao katika mapambano 4.Lango lao wametia nta.

“ndio tuliwakumta waargentia mabao 11,lakini timu nyengine hazikututoa jashi kama wakorea ya kaskazini.” Alisema Birgit Prinz alietia mabao 4 hadi sasa.

Kutamba mechi 4 kwa timu ya Ujerumani bila ya hata kutiwa bao, hakuna kifani chake katika kombe la dunia .Na baada ya kucheza dakika 439 bila kutiwa bao ,wasichana wa Ujerumani wakihitaji dakika 3 za mchezo kuvunja rekodi ya China walioiweka kati ya 1999-2003.

Licha ya matarajio makuu ya kurudi na kombe Berlin, wasichana wa Ujerumani, wanaelewa kitisho cha wanorway,kwani ni wao waliowashinda katika finali ya 1995.Norway wamewashinda wajerumani mara I na wakatokanao sare mwaka huu na watakuwa na hamu kubwa kulipiza kisasi pigo la finali ya 2005.

“Hii ya leo ni nusu-finali itakayochezwa kwa kasi na timu zote mbili, zina nguvu za aina moja na siwezi kubashiri nani ataibuka mshindi.Mshindi ataamuliwa na vitu vidogo-vidogo na bila shaka, matokeo yatakua ya karibu sana.”-alisema kocha wa Norway Bjarne Berntsen.

Alisema kazi yake imekuwa ngumu kutokana na mechi zilivyopangwa kulikoongoza timu yake kucheza mechi 3 mnamo wiki mmoja.

Mpambano dhidi ya Ujerumani utakua mgumu sana.”Sisi tunacheza mechi 3 mnamo wiki 1 wao mechi 3 mnamo siku 10.”-alilalamika kocha wa Norway.

Hii itakua si nafuu kwa wachezaji wake na iliwalibidi kujitahidi sana kuwa fit kwa changamoto ya leo .

Ujerumani na Norway, zimekumbana mara moja tu hapo kabla katika kombe la dunia na hii ilikua finali ya 1995 ambayo Norway, iliibuka mshindi kwa mabao 2:0 na ikatwaa kombe mwaka ule.

Hii ya leo pia ni nusu-finali ya pili pekee kuzikumbanisha timu 2 za Ulaya katika kombe la dunia la wasichana.Katika ile ya kwanza Norway iliilaza Sweden mabao 4-1,1991.

Birgit Prinz,mshambulizi hatari wa Ujerumani anakumbusha kuwa, amecheza mechi nyingi na Norway.Anayoikumbaka sana, ni ile finali ya 1995 na walishindwa na hivyo asema, si ukumbusho mzuri kwa mechi ya leo.

Mara hii lakini anasema Birgit Prinz wanatumai wataondoka china na ukumbusho mwema.

Norway ikiongozwa na mtiaji mabao mengi hadi sasa katika kombe hili la dunia Ragnhild Gulbrandsen namba 5, haikuwahi kushindwa na timu ya Ulaya katika kombe la dunia ,lakini yeye pia anatazamia matokeo leo yatakuwa ya karibu sana. “Tulicheza na wajerumani kabla kuja hapa na tukaotoka nao sare 2:2 na hivyo, tunajua twaweza kuwapa changamoto.” Alisema mshambulizi wa Norway Isabell Herlovsen.

Kwa Ujerumani, lazima ishinde leo,kwani wanaania kuandaa kombe lijalo la dunia mwaka 2011 na wamerefusha mkataba wa kocha wao Neid hadi mwaka huo.Timu nyengine 2 zinazocheza nusu-finali ya pili huko Hangzhou, ni Brazil dhidi ya Marekani.Mshindi wa mpambano huu, atakutana finali na mshindi kati ya Ujerumani na Norway.