1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mahakama ya Ujerumani imemuachia Carles Puigdemont

6 Aprili 2018

Mahakama moja ya Ujerumani imekubali kumuachia huru aliyekuwa kiongozi wa jimbo la Catolonia Carles Puigdemont kwa makosa ya uasi ya kufanya kampeni za kutaka uhuru wa jimbo hilo.

https://p.dw.com/p/2vdHg
Deutschland Neumünster Freilassung Carles Puigdemont
Picha: Reuters/F. Bimmer

 Mahakama hiyo imesema kuwa Puigdemont anaweza kurejeshwa Uhispania na kushtakiwa kwa makosa madogo ya matumizi mabaya ya fedha za umma.

Kiongozi huyo wa zamani wa jimbo la Catolonia alikamatwa mwezi uliopita baada ya Uhispania kutoa waranti wa kukamatwa kwake alipoingia Ujerumani.

Puigdemont apatiwa dhamana na mahakama

Deutschland Neumünster Freilassung Carles Puigdemont
Carles Puigdemont akizungumza na wanahabari Picha: picture-alliance/dpa/A. Heimken

Uamuzi huo unamaanisha kuwa Puigdemont, aliyetoroka Uhispania miezi miwili iliyopita na kuelekea Ubelgiji baada ya waziri mkuu wa Uhispania Mariano Rajoy kupuuzilia mbali utawala wake wa jimbo, hawezi kuhukumiwa kwa uasi nchini Uhispania atakaporejeshwa kwa mujibu wa msemaji wa mahakama ya Ujerumani. Puidgemont amezungumza na wanahabari baada ya kupatiwa dhamana.

"Nataka wenzangu watatu ambao wamefungwa katika gereza la Uhispania wachiwe huru. Ni aibu kwa Ulaya kuwa na wafungwa wa kisiasa. Demokrasia ya aina hiyo ni hatari sana nchini Uhispania."

Msemaji huyo, Frauke Holmer amesema kuwa mahakama sasa lazima iamue kama atarejeshwa uhispania na kushtakiwa kwa matumizi mabaya ya fedha za umma.

Shirika la habari la Reuters lilipouliza mahakama ya Juu na Serikali ya Uhispania iwapo ni sawa kusema kuwa Puigdemont sasa atashtakiwa kwa makosa ya uasi, halikupata jibu.

Uhispania inaheshimu uamuzi wa Ujerumani

Spanien | Regierungssprecher Inigo Mendez de Vigo
Inigo Mendez de Vigo, msemaji wa serikali ya UhispaniaPicha: picture-alliance/dpa/epa/Ballesteros

Mahakama ya Ujerumani ilisema kuwa makosa ya uasi ambayo Puigdemont anakabiliwa nayo sio makosa ya uhalifu nchini Ujerumani, lakini hakuna ushahidi wa kutosha kuhusu suala la machafuko ambalo limehusishwa naye.

Makosa ya uasi yana kifungo cha hadi miaka 25 nchini Uhispania. Mahakama ya Ujerumani imemtoza dhamana ya euro elfu 75 sawa na dola elfu 92

Wakili Wolfang Schomburg ameliambia shirika la habari la Reuters kwa njia ya simu kuwa Puidgemont anajiandaa kuhamisha fedha hizo za dhamana.

Huku hayo yakiarifiwa jaji mmoja nchini Ubelgiji amewapa dhamana waliokuwa mawaziri watatu wa jimbo la Catolonia ambao Uhispania inawataka kurejeshwa nchini humo kuhusu suala tata la uhuru wa jimbo hilo kwa mujibu wa mwendesha mashtaka.

Msemaji wa serikali ya Uhispania Inigo Mendez De Vigo amesema, "Serikali inaheshimu na kuzingatia maamuzi ya mahakama, haijawahi kukiuka athari za maamuzi yake. Puidegemont yuko chini ya mamlaka ya Ujerumani ambayo imebainisha kuwa hajadhulumiwa  kwasababu ya imani yake kisiasa lakini kwasababu ya kutoroka makosa ya uhalifu yanayomkabili."

Watatu hao waliokuwa mawaziri chini ya kiongozi aliyeondolewa madarakani Carles Puigdemont, walijisalimisha katika kituo cha polisi cha Ubelgiji kujibu waranti wa kukamatwa kwao iliyotolewa mwezi uliopita na Uhispania.

Puidgedemont na mawaziri wake wanne walitorokea Ubelgiji mmezi Oktoba mwaka uliopita kuepuka kushtakiwa kwa makosa ya uasi walipokuwa wakitaka jimbo la Catolonia kujitenga na Uhispania.

Mwandishi: Shisia Wasilwa, Reuters, Adp

Mhariri: Josephat Charo