1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yasaidia Ufilipino

12 Novemba 2013

Katika harakati za kuwasaida watu waliofikwa na maafa ya kimbunga cha Haiyan katika kisiwa cha Ufilipino, Ujerumani imepeleka ndege kubwa ikiwa na shehena ya tani 25 za mahitaji muhimu.

https://p.dw.com/p/1AFlM
Waliokumbwa na maafa ya kimbunga Haiyan kisiwani Ufilipino
Waliokumbwa na maafa ya kimbunga Haiyan kisiwani UfilipinoPicha: Reuters/Erik De Castro

Watu zaidi ya alfu 10 wamekufa kutokana na kimbunga Haiyan katika kisiwa cha Ufilipino. Jimbo la Leyte lililopo kati kati ya Ufilipino ndilo hasa lilliloathirika na maafa yaliyosababishwa na dhoruba hiyo. Maalfu kwa maalfu ya watu wanasubiri misaada huku wakiwa katika hali ya kutamauka.

Ndege ya Ujerumani yatua Manila

Licha ya hali ngumu, watoaji misaada kutoka Ujerumani wameshaanza kutoa huduma. Ndege kubwa ya Ujerumani ikiwa na shehena ya tani 25 za misaada imeshatua katika mji mkuu wa Ufilipino, Manila. Ndege hiyo imepeleka mablanketi,mahema, dawa na vifaa kwa ajili ya tiba ya watu waliovunjika mifupa.

Msaada huo umetolewa na mashirika mawili ya misaada ya Ujerumani .Pamoja na shehena ya msaada , Ujerumani pia imewapeleka wataalamu watakaoshughulikia na njia za kuwapatia watu maji safi ya kunywa. Msemaji wa shirika husika la Ujerumani THW Bwana Nicolas Hefner ameeleza kuwa watoaji misaada wa Ujerumani wamegawanyika katika makundi madogo madogo yanayofanya tathmini ya hali katika sehemu mbalimbali zilizokumbwa na maafa.

Matatizo yawakabili watoaji misaaada

Wahanga wa Kimbunga Haiyan wajitahidi kuokowa vilivyobaki
Wahanga wa Kimbuga wajitahidi kuokowa vilivyobakiPicha: Reuters/Erik De Castro

Hata hivyo wanaotoa misaada wanakabiliwa na matatizo kama alivyoeleza Maria Rüther wa shirika la misaada la Ujerumani linaloitwa "Aktion Deutchland Hilft"

Amesema kwa sasa jambo muhimu ni usafirishaji wa mahitaji ya lazima, lakini unakabiliwa na matatizo. Amesema hali hiyo inachelewesha shughuli za usaidizi, na kwa hivyo inabidi kwanza kuviondoa vifusi barabarani ili misaada iweze kufikishwa kwa watu. Kwa sasa misaada inawafikia watu kwa taabu.Njia za mawasiliano zimeharibiwa kwa kiasia fulani.

Kiongozi wa shirika la misaada linaloitwa "Misereor," tawi la Asia Ulrich Füßer amesema kwa sasa mambo yanasonga mbele polepole ,kwa sababu ni vigumu kuitathmini hali yote jumla .Mashirika ya misaada ya Ujerumani yanashirikiana na mashirika mengine kutoka duniani kote. Katika kazi zao watoaji misaada kutoka mashirika ya Ujerumani wanawasiliana na ubalozi wa Ujerumani mjini Manila.

Kwa sasa hakuna anaeweza kutoa tathmini ya uhakika juu ya kiwango cha madhara na kiwango cha misaada inayohitajika.Hata hivyo Maria Rüther wa shirika la "Aktion Deutschland Hilft" amesema mamilioni ya fedha yatahitajika.

Marekani pia yasaidia

Wakati huo huo Marekani imepeleka Ufilipino manowari ya kubebea ndege , USS George Washington na manowari nyingine tano ili kushiriki katika harakati za kuwasaidia watu waliokumbwa na maafa ya kimbunga cha Haiyan.Wizara ya ulinzi ya Marekani imetoaa taarifa hiyo. Hapo awali Marekani ilishatuma wanajeshi na ndege maalumu.

Mwandishi: Kern ,Vera

Tafsiri:Mtullya Abdu.

Mhariri:Josephat Charo