1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ukosefu wa Haki za Wanawake Majumbani

P.Martin9 Agosti 2007

Kwa mara ya kwanza,kuna uwezekano mzuri kwa mwanamke kushinda uchaguzi wa rais nchini Argentina.Lakini usawa wa jinsia majumbani,upo nyuma kabisa.

https://p.dw.com/p/CHjp

Uchunguzi uliofanywa na serikali ya Argentina unaonyesha kuwa wanaume 7 kutoka 10,hawasaidii kazi za nyumbani.Kwa mujibu wa mwanasosiolojia, Eleanor Faur,alie mshauri wa Miradi ya Maendeleo ya Umoja wa Mataifa-UNDP,kuhusu masuala ya wanawake,kiini cha ukosefu wa usawa wa jinsia, katika kila nchi,hata zile za Skandinavia, ni dhamana ya kazi za majumbani.

Tofauti ni kwamba katika nchi zilizoendelea,kuna sera maalum za serikali kubadili mawazo yanayohusu jinsia.Kwa mfano,akina mama na baba waliopata mtoto hupewa mapumziko marefu ya ulezi na vile vile upo uwezekano wa kuwapeleka watoto mahala pa kushinda ua shule za siku nzima.

Lakini nchini Argentina kimila,mfano wa mwanamume kama mtafuta riziki na mwanamke kushughulikia mambo ya nyumbani,umetia mizizi yake katika jamii.

Lakini kasoro inayodhihirika majumbani,ni tofauti kabisa na picha iliyochomoza nchini Argentina majuma ya hivi karibuni.Kwani seneta Cristina Fernande´z ambae ni mke wa Rais Nestor Kirchner, anaongoza katika kura ya maoni kuhusika na chaguzi zitakazofanywa mwezi wa Oktoba nchini humo.

Lakini Faur anasema,wanawake kwa sehemu fulani, wameweza kupata vyeo vya kisiasa kwa sababu ya sheria inayolazimisha vyama vya kisiasa kuwapa wanawake nafasi ya kugombea vyeo.Kwa hivyo,hata majumbani itakuwa shida kupata maendeleo,ikiwa hakutokuwepo sera maalum zinazolenga kubadilisha hali ya mambo majumbani.

Takwimu za mwaka 2001 zinaonyesha kuwa asilimia 42 ya wanawake waliopindukia umri wa miaka 14 hufanya kazi.Wakati huo huo uchunguzi uliofanywa umeonyesha kuwa kwa wastani,wanawake kila siku hufanya kazi kwa saa mbili zaidi kuliko wanaume katika nyumba,ingawa wanawake hao vile vile hufanya kazi nje,sawa na wanaume.

Wanawake wengi wanaofanyakazi nje ya nyumba wanasema,katika uhusiano wa kifamilia huwathamini zaidi wanaume wanaosaidia kugawana kazi za nyumbani au kulea watoto.

Mwanasosiolojia Faur katika ripoti yake juu ya jinsia na haki za binadamu amesema,wazo la “mwanaume wa aina mpya“ ni ndoto ya jinsia mpya. Kwani mabadiliko hayo hutokea miongoni mwa wanaume wachache tu katika baadhi ya familia na si wakati wote au kila mahala.