1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ulimwengu uko wapi kuwalinda raia wa Syria?

Jane Nyingi
26 Oktoba 2016

Huku raia katika mji wa Aleppo nchini Syria wakiendelea kushuhudia mashambulizi ya angani,ardhini na makombora,wengi wanajiuliza ulimwengu umechukua jukumu gani katika kuwalinda raia hao waliochini ya kitisho?

https://p.dw.com/p/2Rjys
Syrien Aleppo - Mitglieder der Civil Defense retten Kinder nach Luftangriff
Picha: Reuters/S. Kitaz

 

Mikataba ya Geneva na ya baraza la usalama la Umoja wa Mataifa ilianzishwa baada ya Vita Kuu ya Pili ili kudumisha amani na kuwalinda watu walio katika maeneo ya vita, lakini mikataba hiyo inaonekana kuwa na ufanisi mdogo. Miongoni mwa mikataba hiyo ya geneva ni pamoja na kanuni ya R2P iliyoanzishwa na mataifa wanachama wa Umoja wa mataifa, ili kuzuia mauji ya halaiki.Ingawa kanuni hiyo ilianza kutumika rasmi mwaka 2005, chanzo chake kilitokana na mauji ya kimbari nchini Rwanda mwaka 1994 ambapo wapiganaji wa kihutu wenye msimamo mkali waliwachinja karibu Wahutu laki nane wengi wao kutoka kabila la wachache la Watustsi na pia Wahutu wenye msimamo wa wastani.

Symbolbild - Ruanda Ladislas Ntaganzwa
Jamii ya kimataifa ililaumiwa kutokana na mauji hayoPicha: picture-alliance/AP Photo/B. Curtis

Kanuni hiyo pia ililenga kuzuia kutokea tena mauji kama ya mwaka 1995, yaliyofanywa na vikosi vya Serbia katika mji wa Srebrenica dhidi ya wanaume na wavulana wa kibosnia elfu 8 wa dini ya Kiislamu .Lakini kanuni hiyo ya umoja wa matifa ya kuwalinda raia inaonekana kutofanikiwa, kwa mujibu wa mbunge wa Uingereza Paddy Ashdown ambae aliwahi kuwa mwakilishi wa juu wa Bosnia na Herzegovina kati ya mwaka 2002-2006.

Ashdown ambae alikuwa miongoni mwa wanasiasa wa Magharibi waliotoa wito wa kuingilia kijeshi vita vya Bosnia katika miaka ya 1990 anasema ulimwengu umekuwa ukisita kujihusisha katika machafuko yanayotokana na migogoro ya muda mrefu.Vita ambavyo vimetokea tangu vile vilivyoongozwa na Marekani nchini Iraq mwaka 2003,vimeonyesha kuwa mataifa ya magharibi hayawezi kuibuka na mikakati mwafaka ya kuwalinda raia, aliongeza mwanasisa huyo wa Uingereza.

Nchini Libya,miaka minane baadae Marekani, Uingereza na washirika wao zimekosolewa kwa kushindwa kuleta amani baada ya kuondolewa madarakani Muammar Gaddafi. Mwaka mmoja uliopita wapiganaji wa kundi linalojiita dola la Kiislamu walichukua udhibiti wa mji Sirte ambao ni makao ya kiongozi huyo wa zamani wa Libya, huku wakiendelea kufaidi kutokana na machafuko yaliotokea baada ya kifo cha Gaddafi mwaka 2011. Mpasuko unaoendelea kukua kati ya Urusi na mataifa ya magharibi uliochangiwa na mzozo mbaya wa mwaka 2014 nchini Ukraine,umeliacha baraza la usalama la umoja wa mataifa kwenye mkwamo katika juhudi za kuleta amani Syria,ambako Urusi inaunga mkono serikali ya Rais Bashar al-Assad.

Syrien Präsident Bashar al-Assad
Rais wa Syria Bashar al AssadPicha: picture alliance/AP Photo/V. Salemi

Kwa mujibu wa Ashton mwanasisa kutoka Uingereza ,ulimwengu umeshindwa kwa mfano kutafuta suluhu ya mzozo wa Libya na Syria.Vita vya Syria vilianza mwaka 2011 kama maandamano ya kupinga utawala wa miongo minne wa familia ya Assad uliochochewa na machafuko yaliyoshuhudiwa katika mataifa ya kiarabu kote mashariki ya Kati.

Israel Panzern-Übung in den Golanhöhen
Vita vinavyoendelea SyriaPicha: picture-alliance/dpa/A. Safadi

Mataifa ya magharibi yanasema serikali ya Syria na mshirika wake Urusi yanakabiliwa na tuhuma za uhalifu wa kivita kwa kuwalenga raia, misaada ya kiutu na hata mahospitali. Hata hivyo mataifa hayo mawili yamekanusha madai hayo na kusema mashmabulizi yao yawanalenga tu wapiganaji. Baada ya kushindikikana makubaliano mawili ya kusitisha vita mji wa Aleppo kati ya Marekani na Urusi,duru mpya ya mazungumzo imepangwa mjini Geneva,Uswisi mwezi huu, na itajumuisha mataifa ya Saudi Arabia na Qatar ambayo yanaunga mkono makundi ya upinzani nchini Syria. Mgogoro wa Syria unaotoa sura ya jinsi migogoro duniani imekuwa migumu kutatulika.

Mwandishi:Jane Nyingi/RTRE

Mhaririri:Iddi Ssessanga