1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Historia

Umesikia nini kumhusu Ahmed Baba

John Juma
25 Julai 2018

Timbuktu uliposhambuliwa, na kudhibitiwa na Sultani wa Morocco, Ahmed Baba alipelekwa Marrakesh ambapo aliruhusiwa kufundisha na kuandika. Ametunga zaidi ya vitabu 50.

https://p.dw.com/p/2phFM

Ahmed Baba alikuwa mmoja wa wanazuoni wakubwawa Afrika katika karne ya 16. Miongoni mwa kazi za mwandishi na mwanachuoni huyo wa Kiislam ni pamoja na maoni yake kuhusu utumwa, wasifu wa wanasheria wanaotajika na sarufi ya Kiarabu. 

Ahmed Baba aliishi wakati gani? Ahmed Baba alizaliwa mwaka 1556. Vyanzo vingine vinaelezea kuwa alizaliwa eneo la Araouane, takriban kilomita 250 Kaskazini Magharibi mwa Timbuktu, mji ulioko magharibi mwa Mali. Hata hivyo kuna uwezekano mkubwa kuwa alizaliwa Timbuktu, kituo kilichokuwa kimepiga hatua kwa mafunzo ya Kiislamu, biashara ikiendeshwa pembeni mwa Kusini mwa Jangwa la Sahara. Baba alifundisha katika misikiti maarufu ya Timbuktu. Baada ya kupinga kushambuliwa kwa Timbuktu mwaka 1591 na Ahmed Al-Mansur aliekuwa Sultan wa Morocco, Ahmed Baba alihamishiwa nchini Morocco. Na huko alikamatwa mateka kwa miaka 12 lakini aliendelea na elimu ya Kiislamu. Ahmed Baba alirejea Timbuktu mwaka 1608 ambapo aliaga dunia 1627. 

Ahmed Baba anafahamika kwa jambo gani? Alipokuwa hai, alijulikana kwa mikataba ya kisheria ambayo ilihusiana na Uislamu na njia nzuri iliyostahili kwa Waislamu kuitumia dini yao. Leo, jina la Ahmed Baba linahusishwa na kumbukumbuku za kipindi cha upeo wa ustawi wa fasihi na sanaa ya Timbuktu. 

Filosofia ya Baba ilikuwa ipi? Ahmed Baba alijitahidi kuleta pamoja makabila tofauti yaliyoishi Timbuktu wakati ule. Kwake, mchanganyiko wa makabila tofauti ulichangia ufahamu ama maarifa. Pamoja na kwamba Wamorocco walimshikilia Baba, walifahamu kuwa alikuwa mwanachuo aliyehitimu. 

DW Videostill Projekt African Roots | Ahmed Baba, Mali
Picha: Comic Republic

Utata uliomwandama Ahmed Baba? Katika makala ndefu yenye mada moja, Ahmed Baba aliandika kuwa Waislamu bila kujali rangi ama asili yao hawawezi kushikiliwa kama watumwa. Wakati huo, watumwa walikuwa moja ya bidhaa za biashara Timbuktu. Ufahamu wake wa sheria za Kiislamu wakati huo, ulionekana kuwa wenye itikadi kali, kwani ulisisitiza usawa kwa Waislamu wote mbele ya Mungu. Hata hivyo, Ahmed Baba hakulaani utumwa, maandishi ambayo yamesalia kuwa halali kwa watu wasio Waislamu.

Kwanini Ahmed Baba angali anapendwa? Ahmed Baba anapendwa kwa usomi wake na hekima, ujasiri wake wa kusema dhidi ya uvamizi wa Wamorocco na upendo wake wa nyumbani kwao, Timbuktu. 

Ahmed Baba anakumbukwa kwa nukuu ipi? Alipokuwa mateka nchini Morocco, Ahmed Baba aliitamani sana nchi yake. "Enyi, mnaokwenda Gao, mfanye hivyo kwa kupitia Timbuktu na mnong'one jina langu kwa marafiki zangu. Wapeni salamu za marashi kutoka kwa mateka ambaye anatamani nchi ambayo marafiki, familia na majirani zake wanaishi."

Asili ya Afrika: Mfahamu Ahmed Baba

Ahmed Baba ameacha kumbukumbu ipi? Taasisi ya Elimu ya Juu na Utafiti wa Kiislamu ya Timbuktu iliyo na miswada 30,000 na moja ya makusanyo ya maandishi ya elimu ya Kiislamu na kubukumbu za kihistoria imepewa jina la Ahmed Baba- amefananishwa na shimo la katikati katika sayari ya zebaki. 

Konstanze Fischer na Philipp Sandner wamechangia katika makala hii. Ni sehemu ya makala maalum za  mfululizo wa "Asili ya Afrika", ushirikiano kati ya shirika la DW na taasisi ya Gerda Henkel.

Mwandishi: Konstanze Fischer na Phillip Sander/Shisia Wasilwa
Mhariri: Mohammed Khelef