1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Ulaya unakaribika mwafaka juu ya mkataba wake

Maja Dreyer15 Oktoba 2007

Baada ya miaka mingi ya vuta ni kuvute kati ya nchi wanachama wa Umoja wa Ulaya juu ya mkataba wa Umoja huu, sasa inaonekana kama makubaliano yanaweza kufikiwa wiki hii. Hilo ni tokeo muhimu la mkutano wa mawaziri wa masuala ya nje wa Umoja wa Ulaya uliofanyika Luxemburg.

https://p.dw.com/p/C7hh
Nchi zipate viti ngani - suali hili bado ni wazi
Nchi zipate viti ngani - suali hili bado ni waziPicha: Photo European Parliament/Architects : Architecture Studio

Mkutano huu wa mawaziri wa nje wa nchi wanachama wa Umoja wa Ulaya ulilenga kutayarisha mkutano wa kilele baadaye wiki hii na kumaliza mivutano iliyobaki.

Na kweli, fursa ni kubwa kwamba mkataba wa Umoja huu unaweza ukapitishwa wiki hii. Matumaini haya anayo waziri wa masuala ya nje wa Ujerumani, Frank-Walter Steinmeier: “Naamini wengi walibadilisha misimamo yao hatua kwa hatua tangu mwanzo mwa mwaka huu. Hii inanifurahisha na pia inanipa moyo kwanza tutaweza kukubaliana katika mazungumzo ya wiki hii.”

Kulingana na waziri Steinmeier, sababu ya kutofikia makubaliano leo ni kwamba mawaziri wenzake wa nchi nyingine hawakupewa mamlaka ya kuamua.

Mkataba huu ambao uliandaliwa baada ya katiba kukataliwa na nchi kadhaa unalenga kuuwezesha Umoja huu kuchukua maamuzi kwa haraka na kulingana na sheria za kidemokrasi. Mfano mada nyingi zaidi zinaweza kukubaliwa kupitia uwingi wa kura kuliko kwa kauli moja tu. Aidha, kura za nchi wanachama zitagawanyika upya kulingana na ukubwa wa nchi.

Poland ilizusha mvutano juu ya idadi za kura, lakini ilipungua dai lake na sasa inataka tu nchi ndogo zipewe haki ya kudai suala lijadiliwe upya ikiwa hazilikubali. Waziri wa nje wa Poland, Bi Anna Fotyga alithibisha kwamba: “Tuko karibu sana kupaka mwafaka.”

Tatizo jingine ambalo bado kutatuliwa ni mgawanyiko wa viti katika bunge la Ulaya ambao unapingwa na Italy. Bunge linatakiwa lipunguzwe hadi viti 750 badala ya viti 785 vilivyoko hivi sasa. Bunge lenyewe lilitoa pendekezo ambalo limeikasirisha Italy, nchi mojawapo kati ya waasisi wa Umoja huu. Kulingana na pendekezo hili, Italy itapoteza viti sita na hivyo haitakuwa na viti sawa na Uingereza na Ufaransa. Kwa mujibu wa wanadiplomasia, waziri mkuu wa Italy, Romano Prodi ataukataa mkataba huo ikiwa suala hilo halitatatuliwa.

Austria na Bulgaria pia zina maombi fulani. Austria inataka kiwekwe kiwango cha juu cha idadi ya wanafunzi wa Ujerumani wanaojiandikisha kwenye vyuo vikuu vya Austria. Na Bulgaria inataka kutumia namna nyingine katika kuandika jina la fedha za Euro ambalo halikubaliwi na benki kuu ya Umoja wa Ulaya.

Haya yote yanatakiwa yatatuliwe hadi mkataba utakapotiwa saini hapo mwezi wa Disemba mwaka huu. Lakini kama mjumbe wa Ureno yenye uwenyekiti wa Umoja wa Ulaya kwa hivi sasa, alivyosema leo, hakuna sababu yoyote kwa nini makubaliano hayawezi kupatikana wiki hii.