1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Ulaya waidhinisha vikwazo dhidi ya Iran na Syria

Prema Martin1 Desemba 2011

Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Umoja wa Ulaya leo mjini Brussels, wamekubaliana kuweka vikwazo vipya dhidi ya Iran na Syria. Lengo ni kuishinikiza Iran kuhusu mradi wake wa nyuklia wenye utata na kuishinikiza Syria.

https://p.dw.com/p/13L29
Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza, William Hague(shoto) na waziri mwenzake wa Uholanzi, Uri RosenthalPicha: dapd

Mawaziri wa nje wa Umoja wa Ulaya katika mkutano huo uliyohudhuriwa pia na Katibu Mkuu wa Umoja wa Nchi za Kiarabu, Nabil al-Arabi, wamekubali kuimarisha vikwazo dhidi ya Syria katika sekta za nishati na fedha, ili kuiadhibu serikali ya Rais Bashar al-Assad inayowakandamiza wapinzani wake. Mawaziri hao, katika taarifa ya pamoja wamesema na ninanukuu: " Umoja wa Ulaya unasisitiza kuwa unalaani vikali, ukandamizaji wa kikatili unaofanywa na serikali ya Syria, ambao unahatarisha kuitumbukiza nchi hiyo katika janga la machafuko, nadharia kali na mapigano ya kimadhehebu." mwisho wa kunukuu.

Mawaziri hao wamekubali kupiga marufuku kuiuzia Syria zana zinazohitajiwa katika sekta ya gesi na mafuta, kununua dhamana za serikali ya Syria na pia kuiuzia nchi hiyo zana za kompyta zinazoweza kutumiwa kudaka mawasiliano ya simu na mtandao. Vile vile wamekubali kusita kuipatia Syria mikopo ya muda mrefu na yenye riba ndogo kuliko ile inayotozwa katika masoko ya fedha. Lengo ni kuinyima Syria uwezo wa kujipatia fedha taslimu. Umoja huo vile vile, umeongeza majina ya watu 12 katika orodha ya wale wanaokabiliwa na vikwazo vya usafiri na waliozuiliwa mali yao. Rais Assad ni miongoni mwa watu 74 waliokuwemo katika orodha hiyo. Makampuni 11 mengine pia yametiwa katika orodha hiyo. Syria imewekewa vikwazo na Umoja wa Ulaya mara tisa. Miongoni mwa vikwazo hivyo ni marufuku ya kuiuzia Syria silaha na kuagizia mafuta kutoka nchi hiyo.

Wakati huo huo, Iran nayo ikiendelea kushinikizwa kuhusu mradi wake wa nyuklia, mawaziri wa nje mjini Brussels, wamekubali kuipanua orodha ya makampuni yanayopigwa marufuku kufanya biashara katika Umoja wa Ulaya kwa kuyataja makampuni mengine 143 na hivyo kufikia 433. Hata idadi ya watu waliopigwa marufuku kuingia Umoja wa Ulaya imeongezeka hadi 113 baada ya majina ya watu wengine 37 kutiwa katika orodha hiyo. Sekta za nishati na fedha pia zitalengwa kwa azma ya kuukwamisha mradi wa nyuklia wa Iran. Kwa mfano, kupiga marufuku kuagizia mafuta kutoka Iran. Waziri wa nje wa Ufaransa Alain Juppe amesema, safari hii wamekubaliana kuchukua hatua kali zaidi dhidi ya Iran.

Mwandishi:Martin,Prema/afpe,afpd

Mhariri: M.Abdul-Rahman