1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Ulaya wasimamisha mazungumzo ya kimkakati ya Urusi

2 Septemba 2008

Urusi imetakiwa kuyaondoa majeshi yake yote kutoka Georgia

https://p.dw.com/p/F90a

BRUSSELS

Viongozi wa umoja wa ulaya waliokutana jana kujadiliana juu ya mzozo wa Georgia wamesimamisha mazungumzo na Urussi juu ya ushirikiano wa kimkakati hadi pale nchi hiyo itakapoyaondoa majeshi yake yote kutoka ardhi ya Georgia kama ilivyokubaliwa katika makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyotiwa saini mwezi uliopita.

Mkutano wa kilele wa Umoja wa ulaya mjini Brussel pia ulilaani hatua ya hivi karibuni ya Urussi ya kutambua uhuru wa majimbo yaliyojitenga na Georgia ya Ossetia Kusini na Abkhazia.

Rais Nicolas Sarkozy wa Ufaransa ambaye ni mwenyekiti wa sasa wa Umoja huo amesema ataongoza ujumbe wa Umoja huo mjini Moscow wiki ijayo.

Kwa upande mwingine umoja huo wenye wanachama 27 ambao unategemea nishati ya gesi kutoka Urusi ulitofautiana juu ya jinis ya kuishawishi urussi kuondoa majeshi yake yote kutoka Georgia.

Wakati huohuo Urusi imesema uamuzi wa umoja wa Ulaya utasababisha majuto. Aidha nchi hiyo imeyaonya mataifa ya magharibi dhidi ya kuiunga mkono kijeshi Gergia na badala yake imezitaka nchi hizo kuiwekea vikwazo vya silaha nchi hiyo hadi pale utawala mpya utakapowekwa madarakani.

Katika mji mkuu wa Georgia Tbilisi mamilioni ya watu walijitokeza kuipinga Urussi.