1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaIsrael

UNRWA: Karibu lita 120,000 za mafuta zahitajika Gaza

Tatu Karema
18 Novemba 2023

Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalowahudumia Wakimbizi wa Kipalestina – UNRWA Juliette Touma amesema lita 120,000 za mafuta zinahitajika kila siku kutoa msaada wa kibinaadamu katika ukanda wa Gaza

https://p.dw.com/p/4Z7gd
Makazi ya muda ya Wapalestina nje ya hospitali ya Al Shifa katika ukanda wa Gaza
Makazi ya muda ya Wapalestina katika ukanda wa GazaPicha: Ahmed El Mokhallalati/REUTERS

Akizungumza na DW kutoka mji mkuu wa Jordan Amman, Touma amesema hawajaweza kuendelea kutoa msaada kwa sababu ya ukosefu wa mafuta na pia kutokana na kukatika kwa huduma za mawasiliano.

Touma amethibitisha kuwa hakuna mafuta yaliyofikishwa Gaza Jana Ijumaa. Baraza la Mawaziri la Israel linaloshughulika na vita hivyo liliidhinisha kuruhusu malori mawili yaliyobeba mafuta kuingia Gaza kutokea Misri kila siku.

Huduma za simu na intaneti zarejeshwa kwa sehemu katika ukanda wa Gaza

Hata hivyo kampuni za mawasiliano ya simu za Paltel na Jawwal zilisema kuwa huduma za simu na intanet zimerejeshwa kwa sehemu katika Ukanda wa Gaza. Zimesema hatua hiyo ilijiri baada ya kuingizwa kwa kiasi fulani cha mafuta kupitia shirika la UNRWA. Shirika la Habari la AFP liliripoti kuwa maafisa wa mpaka wa Gaza walisema lita 17,000 za mafuta zilifikishwa katika ukanda huo jana usiku.