1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Upinzani DRC waitisha mgomo wa kitaifa

Mohammed Khelef
3 Aprili 2017

Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo anatazamiwa kukutana na ujumbe wa upinzani kusaka njia za kuukwamua mkwamo wa kisiasa unaotishia kuyavunja makubaliano ya Disemba 31.

https://p.dw.com/p/2aY2r
Kongo Kinshasa Unruhen wegen Präsident Kabila
Picha: Getty Images/AFP/E. Soteras

Hata hivyo, hakuna uhakika endapo upinzani utashiriki kwenye mazungumzo hayo yaliyoitishwa wakati upinzani nao ukipanga mgomo wa nchi nzima kumshinikiza Kabila kutekeleza kwa vitendo makubaliano hayo yaliyosimamiwa na Kanisa Katoliki nchini Kongo.

Wakati huo huo, mkuu wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Francis, ametoa wito wa kupatikana kwa amani katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, akitaka umwagaji damu ukomeshwe mkoani Kasai.

"Taarifa za mapigano zinaendelea kuwasili kutoka Kasai, ambayo yanapelekea wahanga wengi zaidi na kuwakosesha watu makaazi yao," mkuu huyo wa Kanisa aliwaambia waumini wapatao 2,000 katika mji wa Carpi ulio kaskazini mwa Italia, ambao wenyewe ulikumbwa na matetemeko mawili makubwa ya ardhi mwaka 2012. 

"Kila mmoja aombe ipatikane amani na kwamba nyoyo za wanaohusika na uhalifu huu zisibakie watumwa wa chuki na ghasia," alisema.

Watu wapatao 400 wamekufa ndani ya kipindi cha miezi sita ya machafuko ambayo yamesambaa kwenze majimbo ya Kasai-Central, Kasai, Kasai-West na Lomami.

Vatikanstadt - Papst Franziskus empfängt EU Vertreter
Papa Francis ataka kusitishwa kwa mauaji ya Kasanga, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.Picha: Reuters/Pool/A. Medichini

Mkoa huu unakabiliwa na mapigano tangu vikosi vya serikali kumuuwa kiongozi wa kimila na mkuu wa kundi moja la wanamgambo, Kamwina Nsapu, katikati ya mwezi Agosti 2016. Nsapu anaripotiwa kuanzisha uasi dhidi ya serikali kuu ya Rais Joseph Kabila mjini Kinshasa.

Siku ya Alhamis (30 Machi), viongozi wa kanisa na mwakilishi wa Papa Francis nchini Kongo walivitaka vyombo vya usalama, ambavyo vinatuhumiwa kwa kuwatesa wapinzani, kujizuia kutumia nguvu kupita kiasi wakati wa operesheni zao.

Mwezi uliopita, polisi iliwatuhumu waasi kwa kuwauwa maafisa 39 jimboni Kasai, na wiki iliyopita miilki ya wahandisi wawili wa Umoja wa Mataifa ilipatikana baada ya kutekwa nyara huko Kasai-Central.

Raia wawili wa kigeni walitekwa na watu wasiojuilikana tarehe 12 Machi sambamba na raia wengine wanne wa Kikongo waliokuwa wanawasindikiza.

Bensouda asema uhalifu wa kivita umetendeka DRC

Fatou Bensouda Pressekonferenz
Mwendesha Mashitaka Mkuu wa ICC, Fatou Bensouda, anaamini kuna uhalifu dhidi ya ubinaadamu unatendeka nchini DRC.Picha: picture-alliance/dpa

Katika hatua nyengine, mwendesha mashitaka wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC), Fatou Bensouda, amesema kuuawa kinyama kwa timu ya wataalamu ya Umoja wa Mataifa na ghasia nyengine nchini Kongo kunaweza kuwa sawa na uhalifu unaoweza kushitakiwa na mahakama yake.

Katika taarifa yake ya Ijumaa, Bensouda alisema amesikitishwa sana ghasia kwenye jimbo la Kasai. Miili ya raia wa Marekani, Michael Sharp, Msweden Zaida Catalan, na mkalimani raia wa Kongo, Betu Tshintela, ilipatikana mapema wiki hii. 

Wataalamu hao walikuwa wakichunguza tuhuma za uvunjaji wa haki za binaadamu uliofanywa na jeshi la Kongo na makundi ya wanamgambo kwenye eneo hilo. 

Watu wengine watatu kwenye timu yao, bado hawajuilikani walipo, lakini Bensouda ameitaka serikali ya Kinshasa kufanya uchunguzi wa kina na "wa hakika".  

Kawaida, ICC inaweza kutoa waraka wa kukamatwa kwa washukiwa, lakini ni juu ya taifa mwanachama kuwakamata na kuwafikisha mahakamani kujibu mashitaka.

Mwandishi: Mohammed Khelef/AP/AFP
Mhariri: Iddi Ssessanga