1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Upinzani wasambaratika Ethiopia

Mohamed Dahman18 Oktoba 2007

Wakati kiongozi wa upinzani nchini Ethiopia Hailu Shawel alipoachiliwa huru kutoka gerezani kundi kubwa la jamaa na wafuasi wake lilisogamana kwenye nyumba yake mjini Addis Ababa kuonyesha kipimo cha thamani ya kuwa huru kwake.

https://p.dw.com/p/C7hE
Mji mkuu wa Ethiopia Addis Ababa ni ngome kuu ya upinzani.
Mji mkuu wa Ethiopia Addis Ababa ni ngome kuu ya upinzani.Picha: AP

Inaonekana kwamba wapinzani nchini Ethiopia wamesambaratika licha ya kuachiliwa huru kutoka gerezani.

Kuachiliwa kwa Hailu pamoja na viongozi wengine 37 wa upinzani baada ya kuwa katika gereza lenye ulinzi mkali kwa takriban miaka miwili kwa madai ya kuchochea wafuasi wao kufanya ghasia kupinga matokeo ya uchaguzi uliozusha utata kulipokelewa kwa furaha.

Wafadhili wa mataifa ya magharibi wamepongeza kuachiliwa huko kuwa ni ishara serikali ya Waziri Mkuu Meles Zenawi itafufuwa tena msukumo wake wa kuendeleza demokrasia nchini Ethiopia nchi yenye ushawishi mkubwa katika eneo tata la Pembe ya Afrika na mshirika mkuu wa vita vya kupiga vita ugaidi vya Marekani.

Lakini kwa miezi mitatu sasa Muungano wa upinzani wa Umoja na Demokrasia CDU umegawika na kuvunjwa moyo.Vita vya kupigania mbadiliko nchini Ethiopia badala yake vimekuwa vikiendeshwa na wabunge la Marekani ambao wamepitisha sheria yenye kufungamanisha mageuzi ya demokrasia na msaada wa usalama katika kipindi cha usoni.

Yosef Tesfaye mwalimu wa ushusiano wa kimataifa anasema gereza halikudhoofisha CDU bali wapinzani hao wamejidhoofisha wenyewe kwamba CDU ni mchanganyiko wa makundi mbali mbali, fikra tafauti na watu tafauti kwa hiyo ni dhaifu kwa umbo lake lenyewe binafsi.

Anauona muungano huo unakosa nidhamu ya chama,unakosa mipango,unakosa uongozi na hauwakilishi Ethiopia kama vile inavyodai.

Wataalamu wamekuwa wakiuliza iwapo muungano huo unaweza kujinowa kuwa tayari kwa uchaguzi za serikali za mitaa unaotegemewa kufanyika mapema mwakani.

Maafisa wengi wa CDU akiwemo mwenyekiti wake Hailu na meya mteule wa zamani wa Addis Ababa Berhanu Nega wameondoka Ethiopia kwenda nje kushawishi uungaji mkono wa Waethiopia matajiri wanaoishi nje na kwa upande wa Nega kuwalezea wabunge wa Marekani rekodi ya haki za binaadamu nchini Ethiopia.

Mara tu baada ya kuondoka kwao magazeti ya Ethiopia yameripoti kuwepo kwa mfrakano mbaya kati ya Hailu mwenye msimamo mkali na Nega kijana ambaye shahada yake ya udaktari unaupa mmungano wa CDU sifa zake za usomi.

Wachambauzi hawashangai iwapo maafisa wengine wa CDU wakaacha siasa kwa kutaja sababu za umri au afya mbaya au pengine hata kwenda uhamishoni.

Kwa hivi sasa CDU inalalamika juu ya vikwazo ilivyowekewa kwa harakati zake ambapo ofisi zake za mitaa zimeendelea kufungwa.

Baadhi ya wataalamu wanasema kwamba CDU imekuwa ikivuta wakati ikisubiri maendeleo yatakoyofikiwa katika mazungumzo na chama tawala cha Zenawi ili kujuwa kinaweza kusonga mbele kwa kiasi gani.

Kwani wana hoja ya kuwa na tahadhari.

Wakati wa kuachiliwa kwao Zenawi amesema haki zote za kiraia zitarudishwa kwa viongozi hao wa CDU walioachiliwa huru ikiwa ni pamoja na haki ya kushiriki uchaguzi na wakati huo huo kuwaonya dhidi ya kuchukuwa hatua yoyote ile kinyume na katiba ambayo itawarudisha tena korokoroni.

Hakuna shaka muungano huo wa CDU una uungaji mkono mkubwa katika mji mkuu ambapo ushindi wao mkubwa katika uchaguzi wa mwaka 2005 ulikuwa ni ,kitanzi kwa chama tawala kinachojiamini kupindukia.