1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Upinzani wataka kumshtaki Obama

31 Julai 2014

Baraza la Wawakilishi la bunge la Marekani linaloongozwa na chama cha Republican lapiga kura Jumatano (30.07.2014) kumshtaki Rais Barack Obama kwa madai ya kukiuka madaraka yake ya kikatiba.

https://p.dw.com/p/1CmpD
Rais Barack Obama wa Marekani.
Rais Barack Obama wa Marekani.Picha: Reuters

Baraza hilo limepiga kura 225 dhidi ya 201 kuunga mkono hatua hiyo isio na kifani ya kumburuza rais mahakamani kwa kutotii sheria ipasavyo wakati akiutekeleza muswada wake wa marekebisho ya huduma za afya unaojulikana kama "Obamacare"

Hatua hiyo itamwezesha spika wa baraza hilo la wawakilishi la bunge la Marekani John Boehner kuanza kushughulikia taratibu za kisheria za kumdhibiti rais ambaye amesema amelewa madaraka.

Boehner amesema suala hilo halihusu mvutano kuhusu wabunge wa chama tawala cha Demokrat au Republican bali ni suala la kutetea katiba na kuchukuwa hatua madhubuti wakati katiba hiyo inapohatarishwa.

Kutetea katiba

Amekaririwa akisema "Mko tayari kumuachia rais yoyote yule kuchaguwa sheria gani za kuzitekeleza na sheria gani za kuzibadilisha ? Mko tayari kumuachia yoyote yule kukivunjilia mbali kile kilichojengwa na waasisi wetu ? Msifikirie tu juu ya kiapo mlichokula bali fikirieni jinsi mlivyokula kiapo hicho mkiwa kama chombo kilichosimama pamoja.Hicho ni kitu pekee ninachowaomba leo hii kuitetea katiba kwa niaba ya wananchi tunaowatumikia."

John Boehner Spika wa Baraza la Wawakilishi la Bunge la Marekani.
John Boehner Spika wa Baraza la Wawakilishi la Bunge la Marekani.Picha: picture-alliance/dpa

Boehner amewaambia wabunge wenzake kwamba Obama amekiuka katiba mama ya nchi hiyo kwa kutofuata kikamilifu tafsiri ya kisheria wakati wa kutekeleza marekebisho ya sheria ya afya.

Kwa upande wake Rais Obama amepuuzilia mbali kwa kuikejeli hatua hiyo ya kutaka kumfungulia mashtaka wakati akizungumza kwenye hotuba aliyoitowa huko Kansas City katika jimbo la Missourri.

Amesema huku akishangiliwa na umma uliokuwa ukimsikiliza na kwamba "Badala ya kunishtaki kwa kufanya kazi yangu vizuri, nalitaka bunge kufanya kazi yake kuboresha zaidi maisha ya Wamarekani ambao ndio waliowapeleka bungeni."

Obama pia amewakumbusha wananchi kwamba kwa vyoyote itakavyokuwa ni wao ndio wataobebeshwa gharama za kulipia kesi hiyo mahakamani.

Demokrat yalaani hatua hiyo

Wabunge wa chama cha Demokrat nao hawakupoteza wakati kuilani kura hiyo ya kumfungulia mashtaka rais.

Mbunge mwandamizi wa Demokrat Nancy Pelosi naye ameghadhibishwa na hatua hiyo ya kwanza ya kumshtaki rais katika historia ya Marekani na kumlinganisha na mtu dalimu.

Amesema inatia kichefu chefu, ni siasa chafu na kutomheshimu kabisa rais.

Nancy Pelosi kiongozi wa wabunge wa Demokrat katika Baraza la Wawaklishi la bunge la Marekani.
Nancy Pelosi kiongozi wa wabunge wa Demokrat katika Baraza la Wawaklishi la bunge la Marekani.Picha: AP

Debbie Wasermann Schultz mbunge wa chama hicho kwa jimbo la Florida amesema ni jambo lisilo na tafakuri kwamba wabunge wa Republican baada ya kukosa cha kufanya hatimae wameamuwa kufanya kitu kumshtaki rais kwa kufanya kazi yake wakati wakigoma kufanya yao.

Ameongeza kusema laiti angeliweza kusema hiyo ni siasa chafu kuwahi kuishuhudia na amewataka wapinzani na wabunge wa Republican wasipoteze fedha za walipa kodi kwa azimio hilo na badala yake waungane na wenzao wa Demokrat kushughulikia changamoto nzito zinazoikabili nchi yao.

Mwandishi : Mohamed Dahman/AFP

Mhariri : Josephat Charo