1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Upinzani wataka kususia uchaguzi nchini Nigeria.

Sekione Kitojo18 Aprili 2007

Uchaguzi wa rais nchini Nigeria utakuwa ni hatua ya kwanza ya kubadilishana madaraka kutoka serikali moja ya kiraia kwenda nyingine baada ya miongo kadha ya tawala za kijeshi, lakini wakati muda unakaribia wa uchaguzi , mafanikio yake yanalega lega.

https://p.dw.com/p/CB4d
Bango la uchaguzi linalomwonyesha mgombea Muhamed Buhari katika kuelekea uchaguzi nchini Nigeria.
Bango la uchaguzi linalomwonyesha mgombea Muhamed Buhari katika kuelekea uchaguzi nchini Nigeria.Picha: AP

Uchaguzi wa magavana Jumamosi iliyopita unaonekana kwa kiasi kikubwa kuwa umeendewa kinyume kukiwa na wizi wa kura uliofanywa na chama tawala cha Peoples Democratic PDP, na kusababisha maandamano ya wapinzani nchi nzima.

Mzozo huo umetokana na tangazo la siku ya Jumanne lililotolewa na vyama 18 vya upinzani kuwa watasusia uchaguzi iwapo hautaahirishwa hadi pale uwazi na haki itakapohakikishwa.

Hali hii inaweza kabisa kuelekeza katika mkwamo amesema Chris Albin-Lackey , mtafiti kuhusu Nigeria ambaye anafanyakazi na shirika la kutetea haki za binadamu lenye makao yake makuu mjini New York la Human Rights Watch ambaye alikuwa katika nchi hiyo ya Afrika magharibi yenye utajiri mkubwa wa mafuta lakini masikini.

Nia ya upinzani ni kuonyesha kuwa uchaguzi wa Jumamosi uliendewa kinyume mno, na hakuna sababu ya kufikiri kuwa wanaweza kushiriki katika uchaguzi mwingine mwishoni mwa juma hili.

Wataalamu wanasema kuahirishwa kwa uchaguzi wa hapo Aprili 21 si jambo linalowezekana na mazingira kwa ajili ya uchaguzi huru na wa haki hayapo na hayayawezi kuwepo.

Mwanasheria Mama lawal Yusufari raia wa Nigeria anayeishi nchini Uingereza akizungumza hivi punde na radio Deutsche Welle amesema mazingira ya kuahirisha uchaguzi katika wakati huu ni magumu.

Kwa matokeo ya uchaguzi wa Jumamosi iliyopita , serikali inahisi kuwa na uhakika na inajiamini kuweza kushiriki katika uchaguzi ujao, anasema Nnamdi Obasi , mchambuzi wa kundi la ushauri la kutanzua mizozo la kimataifa. Hali hiyo haitoi uzito kwa upande wa upinzani.

Chama cha PDP kilipata ushindi wa kishindo, kwa kushinda viti 26 kati ya viti 33 vya magavana wa majimbo , ikiwa vipi ni katika jimbo lenye machafuko la Niger Delta, eneo ambalo yanapatikana mafuta mengi ya nchi hiyo.

Kutokana na uchaguzi huo kuwa na uwezekana mkubwa wa kufanyanyika licha ya malalamiko ya upande wa upinzani hasa mtu anayeonekana kuwa katika nafasi nzuri ya kushinda Mohammed Buhari na makamu wa rais Atiku Abubakar miongoni mwa wagombea wengi, nchi hiyo yenye wakaazi wengi katika bara la Afrika na mtoaji mkuu wa mafuta inaelekea kupata serikali ambayo haina uhalali wowote.

Ususiaji mkubwa utakuwa kitu kibaya kabisa. Tutakuwa na uchaguzi ambao utakuwa tu kiini macho kuliko uchaguzi uliopita na serikali itakosa nguvu ya kuwa na uhalali, ameeleza mchambuzi wa masuala ya kisiasa, Obasi.