1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Urusi, China zaikosoa NATO baada ya onyo lake

Iddi Ssessanga
30 Juni 2022

Marekani imeapa kuimarisha ulinzi wa Ulaya kufuatia uvamizi wa Urusi nchini Ukraine, huku jumuiya ya NATO ikiitaja Moscow kuwa kitisho kikubwa zaidi kwa magharibi, na China kuwa changamoto kubwa kwa utulivu wa dunia.

https://p.dw.com/p/4DSoX
China | Wladimir Putin und Xi Jinping
Picha: Aleksey Druzhinin/Sputnik/KremlinREUTERS

Muungano huo wa kijeshi wa mataifa ya magharibi ulikuwa unakamilisha mkutano wake wa kilele hii leo mjini Madrid, ambako umetoa onyo kali kwamba dunia imetumbukizwa kwenye awamu hatari ya mashindano kati ya madola makubwa na vitisho mbalimbali, kuanzia mashambulizi ya kimtandao hadi mabadiliko ya tabianchi.

Viongozi wakuu wa muungano huo wamesema Urusi ndiyo kitisho kikubwa zaidi na cha moja kwa moja kwa usalama wa mataifa washirika na kwa amani na utulivu katika eneo la Ulaya na Atlanki.

Hii imejiri baada ya NATO kuzialika rasmi Sweden na Finland kujiunga na muungano huo, na Rais Joe Biden akitangaza kuongeza wanajeshi wa Marekani, meli na ndege za kivita barani Ulaya.

NATO Gipfel in Madrid
Wakuu wa mataifa ya NATO katika picha ya pamoja wakati wa mkutano wao wa kilele mjini Madrid, Juni 29,2022.Picha: Kenny Holston/Pool/AP/picture alliance

Biden alisema hatua ya Marekani ndiyo hasa ambayo rais wa Urusi hakupenda, na kwamba Moscow ambayo inakabiliwa na upinzani mkubwa kutoka vikosi vya Ukraine vilivyo na silaha kutoka magharibi, ilijibu kwa hasira zinazotabirika.

Rais Putin ameushutumu muungano huo kwa kutaka kueneza ushawishi wake Ulaya, na kuwambia waandishi habari katika mji mkuu wa Turkmenistan, Ashgabat kwamba Ukraine na watu wake ni njia ya NATO kulinda maslahi yake.

Soma pia: Finland yatumai kukubaliana na Uturuki kuhusu NATO

"Ukraine na ustawi wa watu wa Ukraine sio lengo la mataifa ya magharibi na NATO lakini ni njia ya kutetea masilahi yao wenyewe," alisema Putin.

Azionya Sweden na Finland dhidi ya kurusu NATO

Rais Putin pia ameonya kwamba atajibu kwa namna sawa endapo mataifa ya Sweden na Finland yataruhusu majeshi ya NATO na miundombinu ya kijeshi ya muungano huo kwenye ardhi yao, na kuongeza kuwa Urusi italaazimika kuunda vitisho sawa kwa eneo ambalo vitisho dhidi yao vinatengenezwa.

Spanien NATO-Gipfel in Madrid
Rais wa Halmashauri Kuu ya Ulaya Ursula von Leyen akihudhuria mkutano wa kilele wa NATO mjini Madrid, Uhispania, Juni 29, 2022.Picha: Violeta Santos Moura/REUTERS

Hata hivyo waziri mkuu wa Estonia Kaja Kallas, alisema vitisho vya Putin siyo kitu kipya, na kuonyesha mashaka endapo Putin anaweza kuzishambulia Sweden na Finland moja kwa moja.

Lakini alisema wanatarijia matukio ya kustukija kutoka kwa Putin, kama vile mashambulizi ya kimtandao, na vita vya taarifa vinavyoendelea.

China kwa upande wake imeushutumu muungano wa NATO kwa kile ilichokiita mashambulizi ya kuipaka matope nchi hiyo, huku ubalozi wake katika Umoja wa Ulaya ukisema NATO yenyewe ndiyo inasababisha matatizo duniani.

Katibu Mkuu wa NATO Jens Stoltenberg, aliuambia mkutano huo wa kilele kwamba uvamizi wa Urusi nchini Ukraine umesababisha mabadiliko makubwa zaidi katika ulinzi wao wa pamoja tangu kumalizika kwa vita baridi.

Uvamizi huo umesambaratisha kabisaa amani ya Ulaya, na katika kujibu, NATO imemuaga wanajeshi na silaha mashariki mwa Ulaya kwa kiwango ambacho hakijashuhudiwa katika miongo kadhaa.

Chanzo: AFP, DPA, RTRE