1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Urusi yasitisha uhusiano na NATO

Nijimbere, Gregoire22 Agosti 2008

Mgogoro wa Georgia unaelekea kuirudisha dunia katika vita baridi. Urusi imesitisha uhusiano na Shirika la nchi za magharibi NATO baada ya Shirika hilo kufanya hivyo hivi karibuni.

https://p.dw.com/p/F2fp
Rais wa Urusi Dmitry Medvedev na waziri mkuu Vladimir PutinPicha: AP

Katika kile kinachoonekana ni kulipiza kisase, Urusi imesitisha uhusiano wake na Shirika la nchi za magharibi NATO kufuatia mgogoro wa Georgia.

Shirika la nchi za magharibi NATO, limethibitisha kuwa Urusi imesitisha ushirikiano wake na NATO hadi utakapotolewa uamuzi mpya. Msemaji kwenye makao makuu ya Shirika la NATO mjini Brussels Ubelgiji, amewaarifu waandishi wa habari kwamba NATO imejulishwa kupitia idara za kijeshi zinazohusika.

Urusi inazishutumu nchi hizo za magharibi wanachama wa NATO kuegemea upande moja na kuzidi kuiunga mkono Georgia juu ya mzozo wa Ossetia ya kusini na Abkhazia, majimbo ambayo yanapigania kujitenga na Georgia.

Hatua hiyo ya Urusi imechukuliwa siku chache baada ya mawaziri wa mambo ya kigeni wa nchi wanachama wa Shirika la NATO, kukubaliana katika mkutano uliyofanywa mjini Brussels Ubelgiji, kusimamisha uhusiano na Urusi hadi pale nchi hiyo itakapoyaondoa majeshi yake kutoka Georgia kulingana na mkataba wa kusitisha mapigano uliopendekezwa na Ufaransa kwa niaba ya Umoja wa Ulaya.

Urusi imerejelea ahadi yake ya kukamilisha zoezi la kuyaondoa majeshi yake yote kutoka Georgia na kuyapeleka katika jimbo la Ossetia ya kusini hii leo. Shirika rasmi la habari la Urusi Interfax, limemkariri waziri wa ulinzi wa Urusi, Anatoly Serdyukov, kusema kwamba amri imetoka kwa kiongozi mkuu wa majeshi. Hapo kabla, Urusi ilisema inao mpango wa kubakiza wanajeshi wake 500 kwenye mpaka kati ya Georgia na jimbo linalopigania kujitenga na Georgia la Ossetia ya kusini.

Wakati huo huo wizara ya ulinzi ya Marekani, imesema kuwa imewaona wanajeshi wachache mno wa Urusi wakitoka Georgia. Ujerumani imesema Urusi haijapiga hatua ya kuridhisha katika kuyaondoa majeshi yake kutoka Georgia.