1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Usain Bolt awaaga mashabiki wake

Sekione Kitojo
14 Agosti 2017

Usain Bolt awaaga mashabiki wake kwa masikitiko, lakini afurahishwa na hamasa kubwa waliyoonesha mashabiki wake

https://p.dw.com/p/2iD0x
16th IAAF World Athletics Championships London 2017 Usain Bolt
Picha: Getty Images/M. Hangst

Wiki  hii  mashabiki  katika  michezo  ya  ubingwa  wa dunia  walishuhudia  mkimbiaji  maarufu  Usain Bolt akiwaaga  mashabiki , lakini  kwa  masikitiko  makubwa wakati  aliposhindwa  kuanga  kwa  kung'ara , baada  ya kuambulia  medali  ya  shaba  tu  katika  mbio  zake maarufu  za  mika 100  na  pia  kushindwa  kabisa kuambulia  kitu  katika  mbio  za  mita 400  kupokezaja vijiti.

Zaidi  ya  mashabiki  700,000  walijitokeza  katika uwanja  wa  Olimpiki katika  kipindi  cha  michezo  hiyo ikiwa  ni  rekodi  ya  juu  kabisa , na  kuupa  mchezo  huo nguvu  inayohitajika baada  ya  baadhi  kudokeza  kwamba Bolt  pekee ameiweka  michezo  ya  riadha  katika  mwanga katika muda  wa  miaka  iliyopita kwa  kasi  yake  na muonekano  wake. Katika  mkutano  na  waandishi  habari Bolt  alisema.

Großbritannien London: IAAF Weltmeisterschaft: Usain Bolt mit verletzung im Finale
Wachezaji wa mbio za mita 400 kupokezana vijiti wa Jamaica wakimliwaza Usain Bolt kwa kushindwa kumalizia mbio hizo mjini LondonPicha: Reuters/L. Nicholson

"Kwangu  mimi ilikuwa  safi  kabisa, unafahamu  nini ninachomaanisha. Uungwaji  mkono haujabadilika, unafahamu  ninachomaanisha. Nilitarajia  hilo. Inasikitisha kwamba  inabidi  niondoke  hivi  sasa. Lakini  hamasa  ya mashabiki ilikuwa ya  hali  ya  juu  kabisa kama  kawaida na nimewapenda , wamenifanya  nijisikie  niko  nyumbani na kuwa  nakaribishwa. Wapenzi  wangu  kwa  kweli wananipenda na  naikubali  sana  hali  hiyo."

Leichtathletik-WM 100-Meter-Finale
Ishara yake maarufu Usain Bolt aliyokuwa akiwapagawisha mashabiki wakePicha: Reuters/L. Nicholson

Karibu atoke mikono mitupu

Bolt  aliingia  mjini  London  kwa  ajili  ya  mashindano haya  akiwa  na  mataji 11  ya  ubingwa  wa  dunia na dhahabu  8  za  olimpiki  lakini  aliondoka  karibu  mikono mitupu. Alinyakua  shaba  tu  katika  mbio  za  mita  100 na kupata  maumivu  ya  paja  katika  mita  400  kupokezana vijiti.  Na  ameahidi  kwamba  hatarejea  tena  uwanjani kama  mwanariadha na  hajutii  kwamba  hakustaafu mwaka  jana baada  ya  kupata  medali  tatu  za  dhahabu mjini  Rio.

"Kwangu  mimi nilikuwa  nasema  kwaheri  kwa  mashabiki wangu na  nasema tu  kwaheri kwa mbio ninazoshiriki. Hizi ni  mbio  zangu  mbili  ambazo nilidhibiti kwa miaka  kadhaa , kwa  hiyo  nilikuwa  nasema  kwaheri kwa  kila  kitu, mnafahamu  kile  ninachomaanisha. Nafikiri  karibu niangue kilio. Ilikuwa  karibu  lakini  haikufikia  hivyo nilikuwa naaga. Hivyo  ndivyo ilivyokuwa , nilikuwa  naaga matukio ya michezo yangu."

Leichtathletik WM London 2017- Mo Farah
Mo Farah akibusu ardhi baada ya kushinda mbio za mita 10,000 mjini London Picha: Reuters/L. Nicholson

Mbali na  Bolt , Mo Farah  wa  Uingereza pia  alikosa kukamilisha  fainali yake muhumu baada  ya  kushindwa mbio  za  mita 5,000  na  kuambulia  medali  ya  fedha licha  ya  kunyakua  medali  ya  dhahabu  katika  mbio  za mita 10,000.

Caster Semenya  wa  Afrika  kusini  alinyakua  medai  ya dhahabu  katika  mbio  za  800  wanawake , na  hapo kabla  alishinda  mbio  za  mita 1,500.

Mwandishi: Sekione  Kitojo  / afpe /dpae / ape / rtre
Mhariri: Mohammed Khelef