1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ushindi wa Hilary Clinton waathiri chama cha Demokratik

Dreyer, Maja24 Aprili 2008

Mada iliyopewa umuhimu leo katika magezeti ya Ujerumani ni ushindi wa mgombea wa kiti cha urais kutoka chama cha Demokratic cha Marekani, Bi Hilary Clinton.

https://p.dw.com/p/DnwQ
Hillary Clinton jimboni PennsylvaniaPicha: AP

Kwanza ni uchambuzi wa gazeti la “Die Welt”:


“Kwa mara nyingine tena, Hilary Clinton aliweza kubadilisha mwenendo na kuonyesha kwamba bado yungali katika mashindano haya. Katika miezi iliyopita karibu alishindwa na mshindi wake Barack Obama akiwa na mawazo mapya, lakini hata yeye sasa anapata shida kwa sababu hazungumzii vitu vya maana. Tatizo lakini si kwa wagombea bali ni kwa chama cha Demokratik ambacho kinafuatia kwa hofu kubwa mashindano yanayoendela kati ya wagombea hao wawili. Mwaka mmoja ulipita hakuna aliyeamini mgombea wa Republikan ataweza kushinda, lakini kutokana na mgogoro ndani ya chama cha Demokratik, John McCain wa Republikans anazidi kuwa na nafasi ya kushinda uchaguzi wa urais.”


Gazeti la “Tageszeitung” la mjini Berlin linachambua udhaifu wa Barack Obama. Limeandika:


“Ushindi wa Hilary Clinton katika majimbo ya Ohio na Pennsylvania unaweka wazi wapi Obama anashindwa, yaani kutoungwa mkono na wapigaji kura wa tabaka la kati la Wazungu na wafanyakazi wa kawaida wa Kizungu. Hiyo inawapatia changamoto kubwa wale wajumbe maalum 795 ambao baadaye mwaka huu wataamua mgombea gani atapigania urais kwa tiketi ya chama chao cha Demokratic. Hilary Clinton anafanya kila awezalo kupata ushindi hata ikiwa chama chake kitaathirika.”


Tukiendelea na gazeti jingine kubwa la Ujerumani, yaani “Frankfurter Allgemeine Zeitung” nalo linaona vilevile kuwa chama cha Demokratik kinaachwa nyuma na chama cha Republikan kuhusiana na uchaguzi wa urais. Tunasoma:

“Bila ya kujali nani atateuliwa kupigania wadhifa wa urais kupitia tiketi ya chama cha Demokratik, ikiwa ni Bw Obama au Bi Clinton, jukumu lake kubwa litakuwa kuunganisha tena sehemu mbili za chama hiki zilizotengana. Haijulikani ikiwa wafuasi wa Bi Clinton katika uchaguzi mkuu watamchagua Obama ambaye anataka kuleta mabadiliko – na kinyume chake. Mpaka sasa ni John McCain wa Republikans ambaye ananufaika kutokana na mashindano haya.”


La mwisho katika  udondozi huu wa leo ni mada nyingine ambayo inazungumziwa na wahariri mara kwa mara wiki hii, yaani mzozo wa chakula duniani. Jana bunge la Ujerumani liliamua kuongeza misaada ya vyakula. Licha ya hayo lakini, mhariri wa “Stuttgarter Zeitung” anaiona changamoto nyingine. Ameandika:

“Suali muhimu ni misaada hii itatumika vipi? Kwanza bila shaka ni msaada wa dharura, lakini ili kujipanga kwa siku za mbele lazima sera za maendeleo zirekebishwe. Umuhimu ulipewa hasa kwa miradi ya kujenga mifumo ya kidemokrasi na utawala wa kisheria, mambo ambayo kweli ni muhimu katika kutokomeza rushwa na mizozo, lakini wakati huo huo maeneo yaliyo mbali na miji mikubwa yalisahauliwa. Huko lakini mashambani ambapo chakula  kwa watu wengi kinatengenzwa, njaa ni kubwa mno.”