1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Utafiti: China ni mshirika mkubwa wa Afrika kiuchumi

John Juma
28 Juni 2017

China ni mshirika mkubwa wa Afrika kiuchumi. Hata hivyo kumekuwa na changamoto kufahamu kwa kina ushirika huo kutokana na taarifa zilizopo. Ripoti mpya ya utafiti uliofanywa na shirika la McKinsey imesema.

https://p.dw.com/p/2fXi6
Südsudan Ausländische Arbeiter Chinesen
Picha: picture-alliance/Imaginechina/Tong Jiang

China ni mshirika mkubwa wa Afrika kiuchumi. Hata hivyo kumekuwa na changamoto kufahamu kwa kina ushirika huo kutokana na taarifa zilizopo. Ripoti mpya ya utafiti uliofanywa na shirika la McKinsey Africa imegundua kuwa ushirika wa China ni mkubwa zaidi kuliko namna ambavyo ripoti za awali zilionesha.

Kufuatia utafiti uliofanywa katika nchi nane, ambazo kwa pamoja huunda theluthi mbili za mapato jumla ya nchi za ukanda wa kusini mwa jangwa la Sahara, ripoti iligundua kuwa tayari yapo zaidi ya makampuni 10,000 ya China, yanayofanya kazi barani Afrika. Hiyo ikiwa ni mara nne zaidi ya makadirio ya awali.

Takriban asilimia 90 ya kampuni hizo ni zile za binafsi katika sekta tofauti tofauti na za viwango mbalimbali, huku theluthi moja zikijikita katika viwanda. Kampuni hizo zinachangia kwa mitaji ya uwekezaji, maendeleo ya usimamizi na ujasiriamali katika sekta ya nishati katika bara la Afrika. Kwa kufanya hivyo, zinasaidia kukuza maendeleo ya uchumi wa nchi za Afrika. Omid Kassin ni Mshirika Mkuu wa utafiti huo uliofanywa na shirika la McKinsey na anasema yapo matumaini zaidi ya ushirikiano huo kuimarika hata zaidi.  "Tunaamini kuna nafasi ya kuendelea zaidi. Kwa sasa thamani ya biashara katika bara la Afrika ni takriban dola bilioni 180. Tunaamini hilo linaweza kuongezeka hadi dola bilioni 440 ifikapo mwaka 2025."

Ujenzi wa reli nchini Kenya uliofanywa na kampuni ya China
Ujenzi wa reli nchini Kenya uliofanywa na kampuni ya ChinaPicha: Reuters/N. Khamis

Ufadhili wa miradi na biashara

Katika sekta za biashara, uwekezaji, miundo mbinu, fedha na misaada, China ni namba moja miongoni mwa nchi nyingine tano zenye ushirika na Afrika, wala hakuna nchi inayoweza kulingana na kiwango chake cha ushirika. Kutokana na hali hiyo, biashara imeinuka kwa asilimia 20 kila mwaka, katika kipindi cha mwongo mmoja uliopita.

Fedha zinazotoka China kuelekea Afrika ni asilimia 15 zaidi ya fedha rasmi zinazotajwa wakati masuala mengine tofauti na ya zamani yanapojumuishwa. China pia imeimarika kuwa mshirika mkubwa wa misaada na pia mfadhili mkuu wa fedha katika kutekeleza miradi mingi ya miundo mbinu ambazo zimeshuhudiwa Afrika katika miaka ya hivi karibuni.

Kando na viwanda, robo ya kampuni za China zimejikita katika utoaji huduma na khumusi kwenye biashara na ujenzi. Tayari asilimia 12 za mapato ya viwanda va Afrika hutokana na kampuni za China, hiyo ikikadiriwa kuwa ni jumla ya dola bilioni 500 kwa mwaka.

Bango la kampuni ya China inayojenga reli Kenya
Bango la kampuni ya China inayojenga reli KenyaPicha: Reuters/N. Khamis

Malengo ya kudumu ya kampuni za China

Katika miundombinu, China imechukua asilimia 50 ya soko la Afrika kuhusu uhandisi, ununuzi na ujenzi. Kampuni za China zinapata faida nzuri. Karibu robo ya kampuni 1000 zilizoshirikishwa kwenye utafiti zilisema zimeweza kurejesha fedha zao za mtaji kwa muda wa mwaka mmoja au chini ya muda huo, huku theluthi moja ikisema ilipata faida ya zaidi ya asilimia 20.

Zinalenga zaidi matakwa ya masoko ya Afrika yanayokuwa kwa kasi kuliko kulenga kwenye bidhaa za kuuza au kusafirisha nje ya Afrika. Uwekezaji wao unaashiria ushirikiano wa kudumu kwa Afrika. Katika kampuni za China zilizohojiwa, asilimia 74 ilisema zina matumaini ya mustakabali mzuri wa Afrika.

Ripoti hiyo inadokeza faida tatu kuu za kiuchumi kutoka China kwa Afrika kutokana na uwekezaji na biashara. Kubuni nafasi za ajira na taaluma. Pili kubadilishana ujuzi na teknolojia na tatu ufadhili na maendeleo ya miundo mbinu.

Mwandishi: John Juma

Mhariri: Josephat Charo