1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uturuki mwaka mmoja tangu jaribio la mapinduzi

Sekione Kitojo
15 Julai 2017

Uturuki leo(15.07.2017)Jumamosi itakuwa na matukio mbali mbali ya sherehe za kumbukumbu ya mwaka wa kwanza baada ya kushindwa kwa jaribio la mapinduzi mwaka jana,rais Recep Tayyip Erdogan alionesha anadhibiti madaraka.

https://p.dw.com/p/2gaZz
Türkei Putschversuch
Picha: picture-alliance/dpa/S. Suna

Maafisa  wameitangaza  siku  ya  Julai 15 kuwa  siku  ya   sikukuu ya  kitaifa  ya "demokrasia na umoja", kwa kuonesha  kwamba kuzuiwa kwa  mapinduzi ni  ushindi  wa  kihistoria  kwa  demokrasia nchini  Uturuki.

Watu 249 , bila  la  kujumuisha  waliopanga  njama  hizo , waliuwawa wakati  kikundi  ambacho  hakikubaliani na  hali  ya  mambo  katika jeshi  kilituma  vifaru  mitaani  pamoja  na  ndege  za  kijeshi  hewani katika  jaribio  la  matumizi  ya  nguvu  kumuondoa  madarakani Erdogan  baada  ya  muongo  mmoja  na  nusu  madarakani.

Türkei Putschversuch
Usiku wa mapinduzi watu walijikusanya katika daraja la Bosphorus mjini Istanbul kuzuwia jaribio la mapinduziPicha: picture-alliance/abaca/F. Uludaglar

 

Lakini jaribio  hilo  lilizuiwa  katika  muda  wa  masaa  machache wakati  maafisa  walipojipanga  na  watu kumiminika  mitaani kumuunga  mkono  Erdogan, ambaye  aliwalaumu wafuasi wa mshirika  wake  ambae  aligeuka  kuwa  hasimu, imamu anayeishi uhamishoni  nchini  Marekani Fethullah Gulen , ambaye  anakana kuhusika.

Bila  ya  kusita , maafisa  walianza  kuwakamata  watu wanaoshukiwa  kuhusika  na  jaribio  hilo  katika  operesheni  kubwa kabisa  kuwahi  kutokea  nchini  Uturuki, na  kuwakamata  watu 50,000 na  kuwafukuza  kazi  zaidi  ya  watu  wengine 100,000. Erdogan  pia  alijiimarisha  katika  nafasi  yake kwa  kushinda  kura ya  maoni  hapo  Aprili 16 , akiimarisha  madaraka  yake.

Türkei Recep Tayyip Erdogan in Istanbul
Rais wa Uturuki Recep Tayyip ErdoganPicha: Reuters/M. Sezer

Kiwango  cha  maadhimisho  ya  leo Jumamosi  nchi  nzima kinalenga  katika  kuiweka  Julai 15 kusalia vichwani  mwa  Waturuki  kama siku ya  kihistoria  ya  taifa  la  kisasa  lililoasisiwa  mwaka  1923 kutoka  katika mabaki  ya  himaya  ya  Ottoman.

"Kuanzia  sasa  na  kuendelea,  hali  haitakuwa  tena  kama ilivyokuwa  kabla  ya  Julai 15," Erdogan  alisema  katika  hotuna siku  ya  Alhamis.

Mabadiliko ya  kihistoria

Alilinganisha  kushindwa  huko kwa  jaribio  la  mapinduzi  na mapigano  katika  vita  vikuu vya  kwanza  vya  dunia  mwaka  1915 katika  eneo  la  Gallipoli  ambapo  vikosi  vya  Ottoman  viliweza kuhimili  mashambulizi  ya  wanajeshi  wavamizi  wa  muungano katika  kile  kilichokuja  kuwa  moja  kati  ya  simulizi  za  taifa  la kisasa.

Berlin Tag der Pressefreiheit
Maandamano mjini Berlin yakitaka waachiliwe watu waliokamatwa nchini UturukiPicha: Imago/Müller-Stauffenberg

"Mataifa yana sehemu  muhimu  ya  mabadiliko  katika  historia  yake ambayo  inaunda  mustakabali  wa  baadaye. Julai 15 ni  siku  kama hizo  kwa  jamhuri ya  Uturuki,"  amesema.

Mabango  makubwa  yaliyotengenezwa  na  rais  yamezuka  katika maeneo  mbali  mbali  ya  matangazo  makubwa  mjini  Istanbul yakionesha  michozi maridadi  ambayo  inaonesha  matumio  muhimu katika  usiku  huo  wa  mapinduzi, ikiwa  ni  pamoja  na  kusalimu amri  kwa  wanajeshi  walioendesha  jaribio  hilo  la  mapinduzi. 

"Kilele cha  Julai 15,"  inasema  kauli  mbiu.

Upinzani walalamikia ukandamizaji

Upinzani  nchini  Uturuki  umeweka  tofauti  za  kisiasa  kando  katika usiku  wa  jaribio  la  mapinduzi. Lakini  hali  hii  imeyeyuka  tangu kura  ya  maoni  ya  tarehe  16 Aprili, ambapo  wakosoaji wanamshutumu  Erdogan kwa  kutafuta  kuwa  na  utawala  wa  mtu mmoja  na  kukandamiza  mtu  yeyote ambaye  anaelezea kutoridhika  kwake.

Katika hatua  ya  hivi  karibuni, maafisa  siku ya  Ijumaa walitangaza kufutwa  kazi  kwa  wanajeshi  zaidi, polisi ,  na  maafisa 7,563, ambapo  karibu  wanajeshi 350  waliokwishastaafu  walivuliwa  vyeo vyao.

Thousands Mass To Mark Anti-Erdogan Rally - Istanbul Kemal Kilicdaroglu  Selvi Kilicdaroglu
Wapizani wanataka kurejeshwa kwa demokrasia halisi nchini UturukiPicha: picture alliance/abaca/Depo Photos

Ikija  katika  mkesha  wa  maadhimisho , taarifa  ilisema  wale waliolengwa  walikuwa  "wanahusika  na   makundi  ya  kigaidi, ama makundi ambayo  yana  nia  ya  kuchukua  hatua  dhidi  ya  usalama wa  taifa".

Mapema  mwezi  huu  Uturuki  pia  iliwatia mbaroni  mkurugenzi  wa shirika  la  kutetea  haki  za  binadamu  nchini  humo  la  Amnesty International  pamoja  na  nusu  dazeni  ya  watetezi  wa  haki  za binadamu  kwa  madai  ya  kuhusika  na  kundi  la  kigaidi. Uturuki inaendelea  kuwa  chini  ya  hali  ya  hatari  iliyowekwa  Julai 20, ambayo  imerefushwa  mara  tatu.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / afpe

Mhariri: Caro Robi