1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uzazi wa siri nchini Germany

Zainab Aziz
13 Julai 2017

Sheria ya kuzaa kwa siri nchini Ujerumani ilipitishwa miaka mitatu iliyopita. Wanawake zaidi ya 300 wameitumia sheria hiyo na wamewazaa watoto wao kulingana na sheria hiyo ya kujifungua bila kujulikana. 

https://p.dw.com/p/2gUzT
Schwangerschaft - Übelkeit
Picha: Colorbox

Ni hali ngumu kwa mwanamke ambaye ni mjamzito na hataki mtu yeyote ajue linapokuja swala la kuzaliwa kwa mtoto wake hasa pale anapohitaji kujificha mimba hiyo kutoka kwa wazazi wanaowatesa au waume wanao wanaowadhalilisha. Wanawake wanakuwa na hofu na hawataki majina yao au anwani ya hospitali wanayojiandaa kwenda kujifungua ijulikane.

Mnamo mwezi Mei mwaka 2014 serikali ya Ujerumani ilianzisha sheria inayotoa fursa ya uwezekano wa wanawake kuweza kujifungua kwa siri ili kuwasaidia wanawake wanaohusika. Chini ya sheria hiyo mwanamke anaweza kupiga simu ya bure, saa ishirini na nne katika siku saba za wiki bila ya kuwepo ulazima wa kujitambulisha na atakuwa na haki ya kupata msaada mara moja ambapo wataalamu watahakikisha anapelekwa kwa mshauri wa karibu. Iwapo mwanamke mjamzito ataamua kwamba anataka kujifungua mtoto wake kwa siri anaweza pia kupata msaada wa kifedha anaohitaji na kuzaa katika hospitali au kwa mkunga bila ya kutoa kitambulisho chake. Mtoto aliye zaliwa mara nyingi huwekwa katika huduma ya serikali na hutunzwa huku akisuburi mzazi au wazazi walezi.

Deutschland Nationaler Aktionsplan gegen Rassismus
Waziri wa Ujerumani wa familia na wanawake Katarina BarleyPicha: picture-alliance/dpa/K. Nietfeld

Miaka mitatu baadaye, tangu sheria hiyo ilipoanzishwa kitengo cha huduma ya familia cha nchini Ujerumani kimewasilisha utafiti juu ya tathmini ya sheria hiyo. Tangu sheria hiyo ilipoanzishwa mnamo mwezi Mei mwaka 2014 wamezaliwa watoto 335 ikiwa ni zaidi ya watoto 100 kwa kila mwaka. Daktari Jörn Sommer, aliyeongoza utafiti juu ya sheria iliyopitishwa na serikali ya Ujerumani, anasema wengi kati ya wanawake wajawazito ambao wanataka kuweka siri mimba zao pamoja na wakati wa kujifungua huchagua hatua hiyo ya kuzaa kwa siri kama njia mbadala ambapo mzazi anaweza kumwondoa na kumpekeleka mtoto wake mahala popote bila kujulikana na mtu yeyote.

Hata kabla ya sheria hiyo kupitishwa miaka mitatu iliyopita, kulikuwa na idadi ya vituo  vinavyojulikana kwa kuwapokea watoto, au vyumba vya kuwaacha watoto kwa siri nchini Ujerumani. Hivi ni vyumba ambavyo kwa kawaida huunganishwa na hospitali, ambapo mama aliye kata tamaa anaweza kumweka mtoto mchanga bila kuwasiliana na mtu yeyote. Mara tu mtoto akiwekwa kwenye kitanda kidogo kengele hulia na wahudumu huenda kumchukua mtoto mchanga aliyeaachwa.

Kwa ujumla, sheria hii ni muhimu sana kwa sababu inasaidia wanawake walio katika hali ngumu  Katharina Jeschke, mwanachama wa bodi ya usimamizi wa chama cha wakunga ameiambia DW kwamba chama chake kinahakikisha kuwa wanawake wanapokea msaada wa matibabu na kisaikolojia wakati wa ujauzito na baada ya kujifungua, pia chama hicho kimezisaidia hospitali na wakunga katika maswala ya kisheria wakati mwanamke mjamzito alipotaka kuhifadhi jina lake libakie siri kabla ya kujifungua.

Licha ya yote hayo, uzazi wa siri unahitaji wanawake kupitia mchakato maalum ambao ni pamoja na kutumia vitambulisho vyao kwa ajili ya kujiandikisha kwa mshauri.

Mwandishi: Zainab Aziz/dw.com/p/2gQ1S

Mhariri:Iddi Ssessanga