1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Van Gaal akasirishwa na waandishi wa habari

24 Desemba 2015

Kocha wa Manchester United Louis van Gaal amezungumza kwa ghadhabu wakati wa kikao cha waandishi wa habari kabla ya mchuano ujao wa ligi kuu ya Premier dhidi ya Stoke City.

https://p.dw.com/p/1HSdt
Großbritannien Manchester United Trainer Louis Van Gaal
Picha: picture-alliance/dpa/N. Roddis

Van Gaal anayekabiliwa na shinikizo kubwa kutokana na matokeo mabaya ya timu yake, aonekana kukasirishwa kutokana na uvumi unaoendelea kusambaa katika vyombo vya habari kuwa anaeleeka kupoteza nafasi yake ya ukufunzi katika klabu hiyo. Ripoti za Vyombo vya habari zinasema kuwa Van Gaal anakabiliwa na mtihani mkubwa wa kuifufua timu yake la sivyo huenda akapigwa kalamu, huku aliyekuwa kocha wa Chelsea Jose Mourinho akiwa mmoja wa majina yanayopigiwa upatu kuchukua nafasi hiyo.

Habari hizo zimemkasirisha Van Gaal, ambaye jana amewaambia waandishi wa habari, kuwa alitarajia wamwombe radhi kutokana na ripoti za ‘uwongo‘ walizochapisha. Mholanzi huyo alikiri kuwa na namnukuu “sasa hatupo kwenye nafasi nzuri lakini kumbukeni Wiki nne zilizopita tulikuwa Namba moja kwenye Ligi na baada ya Wiki nne tunaweza kuwa wa Kwanza tena“.

Baada ya dakika nne tu, Van Gaal alimalizia hotuba yake kwa kuwaambia waandishi “nawatakia Krismasi njema na Mwaka Mpya mwema, ikiwa tutaonana tena, na Furahieni Mvinyo na Mikate pamoja na Nyama ya Kusaga“. Hapo akaondoka na kwenda zake.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP
Mhariri: Mohamed Khelef