1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vettel aifikia rekodi ya Schumacher katika F1

4 Novemba 2013

Bingwa wa dunia Sebastian Vettel bado hajamaliza kurarua kurasa za madaftari ya kumbukumbu na rekodi katika mbio za magari ya Formula One, baada ya kushinda mbio za Abu Dhabi Grand Prix

https://p.dw.com/p/1ABNU
Picha: Getty Images

Ushindi wake mkubwa hapo jana katika mkondo wa Abu Dhabu Grand Prix ulikuwa wa saba mfululizo, kwa kuifikia rekodi iliyowekwa na Michael Schumacher mwaka wa 2004, na wake wa kumi na moja msimu huu ambao unamweka kileleni akiwa na pengo la pointi 130 mbele ya mpinzani wake wa karibu Fernando Alonso wa kikosi cha Ferrari.

Dereva huyo mjerumani mwenye umri wa miaka 26 wa kikosi cha Red Bull ndiye bingwa mwenye umri mdogo zaidi kuwahi kushinda mataji manne ya ulimwengu katika Formula One, na kufikia mwishoni mwa mwezi huu, huenda akazifikia rekodi nyingine mbili. Huku ikiwa imesalia mikondo miwili msimu kukamilika, huenda akaifikia rekodi iliyowekwa na Schumacher ya kushinda mikondo 13 katika msimu mmoja, na ya Alberto Ascari ya ushindi mara tisa mfululizo katika msimu mmoja.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/Reuters

Mhariri: Yusuf Saumu