1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi wa Afrika watoa mpango wa usuluhishi Libya

2 Julai 2011

Viongozi wa Afrika wamekubaliana jana Ijumaa kuhusiana na mpango wa amani ambao unamuweka kando ya mazungumzo kiongozi wa Libya kanali Muammar Gaddafi.

https://p.dw.com/p/11nix
Kanali Muammar Gaddafi ambaye umoja wa Afrika unataka asihusishwe katika mazungumzo ya kuleta amani.Picha: picture alliance/dpa

Viongozi  wa  Afrika   wamekubaliana  jana  Ijumaa  kuhusiana  na mpango  wa  amani  ambao  unamuweka  kando   ya   mazungumzo kiongozi  wa  Libya, kanali  Muammar Gaddafi  na  waasi. Mpango huo  tayari   umewasilishwa  kwa  pande  zote  kwa  matumaini  kuwa unaweza  kuelekeza  katika   hatua  ya  mazungumzo. 

Mpango  huo  unajumuisha  Gaddafi  kutoa  ahadi  ambapo  atakubali hatua  za  majadiliano , na  kukubali  kwake   kuwa   hatakuwa sehemu  ya   hatua  ya  majadiliano, kwa  mujibu  wa   waraka  huo. Mpango  huo  hautoi  wito  kwa  Gaddafi  kujiuzulu,  ambalo  ni  dai kuu  la   waasi  katika  baraza  la  taifa  la  mpito  ambalo  limesisitiza katika  mkutano  huo  kuwa  Gaddafi  ni  lazima  aondoke kwa vyovyote  vile, hata  kama  utapatikana  muafaka  wa  kisiasa  katika mzozo  huo  uliodumu  miezi  minne  sasa.

Mkutano  huo  wa  kilele  pia  umeamua  kutotekeleza  waranti uliotolewa  na  mahakama  ya  kimataifa   ya  uhalifu   dhidi  ya Gaddafi, mtoto  wake  na  mkuu  wa  idara  ya  upelelezi , ambao wamesema  unatatiza  juhudi  za  kuleta  suluhisho.

Jubel Internationale Strafgerichtshof Gaddafi Libyen
Waasi wa Libya wakishangiria baada ya kupata taarifa ya waranti uliotolewa na mahakama ya kimataifa dhidi ya GaddafiPicha: dapd

Tumepata  fursa  muda  mfupi  uliopita  kukabidhi  rasmi  kwa  ujumbe wa  pande  zote  mapendekezo  yetu  ili  wayapeleke  kwa  wenzao, rais  wa  Afrika  kusini  Jacob Zuma  amewaambia  waandishi habari. Ameongeza  kuwa  wamepokea  mapendekezo  hayo  kwa moyo  mkunjufu. Tuna  furaha  kuwa  tumefikia  katika  hatua  hii, ambayo  tunaweza  sasa  kusema  hivi  karibuni  tutaanzisha mazungumzo  mjini  Addis Ababa  na  tunaamini  tutapata  uungwaji mkono  kutoka kwa  kila  mmoja, amesema  rais Zuma.

Südafrika Parlament wählt neuer Präsident Jacob Zuma
Rais wa Afrika kusini Jacob Zuma amesema kuwa anamatumaini hivi karibuni mazungumzo ya amani nchini Libya yataanza mjini Addis AbabaPicha: AP

Mpango  huo  unatoa  wito  wa  kusitishwa  mara  moja  mapigano, usitishaji  wa  hali  ya  kiutu, usitishaji  kamili, maridhiano  ya  kitaifa, mipango  itakayohusiana  na   hatua  za  mpito, pamoja  na  angenda kwa  ajili  ya  mabadiliko  ya  kidemokrasia. Miji  yote  ni  lazima iachwe  huru  bila  kuzingirwa  na  majeshi, mashambulio  yasitishwe na  watu  ambao  wamekamatwa  wakati  wa  mzozo  huo  waachiwe huru, umeeleza  waraka  wa  mpango  huo.

Pia  waraka  huo  umeeleza  kuwa  umoja  wa  mataifa  unapaswa kuondoa  marufuku  ya  kuruka  ndege  za  Libya  katika  anga  lake, hatua  ambayo  imesababisha  mashambulio  yaliyoongozwa  na NATO dhidi  ya  majeshi  ya  Gaddafi, na  umoja  wa  Afrika  pamoja na  jumuiya  ya  mataifa  ya  Kiarabu , zitatuma  vikosi  vya  kutosha vya  jeshi  la  kulinda  amani.

Mpango  huo  pia  unaeleza  kuwa  kipindi  cha  mpito  kitajumuisha siku  30  za  majadiliano  ya  kitaifa,  ambayo  yataelekeza   katika uchaguzi  na  pia  kuruhusu  msamaha .

Jumuiya  ya  kimataifa  itachunguza  juu  ya  kutimizwa  kwa usitishaji  wa  mapigano,  kuondoa  vikwazo  na  kuondoa  hatua   ya kuzuwia  mali  za  Libya  nchi  za  nje. Lakini  ujumbe  wa  waasi umesisitiza  siku  ya  Alhamis  kuwa  ili  mazungumzo  yoyote yaanze, Gaddafi  ni  lazima  aondoke, dai  ambalo  maafisa  wa umoja  wa  Afrika  wamesema  linaweza  kuletwa  katika  meza  ya majadiliano. Mwakilishi  wa  baraza  la  taifa  la  mpito  Mansour Safy al-Nasr  amesema   kuwa  waasi  wataendelea  kupigana  hadi  pale Gaddafi  atakapoondoka, lakini  pia  watasitisha  mapigano  iwapo ataondoka.

Iwapo  tutaona  kuwa  Gaddafi  anajiondoa , tuko  tayari  kuacha mapigano  na  kujadiliana  na  ndugu  zetu  ambao  wako  karibu  ya Gaddafi, amesema  Nasr.

Guido Westerwelle und Mahmud Jibril Berlin Deutschland
Mwenyekiti wa baraza la mpito nchini Libya akizungumza na waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani Guido WesterwellePicha: dapd

Kiongozi  wa  ngazi  ya  juu  wa  waasi  nchini  Libya  Mahmud Jibril amewataka  viongozi  wa  umoja  wa  Afrika  kuchukua  msimamo uliowazi   dhidi  ya  Gaddafi  baada  ya  mahakama  ya  kimataifa  ya uhalifu  kutoa  waranti  wa  kukamatwa  Gaddafi  siku  ya  Jumatatu. Lakini  mkutano  huo  umeamua  kuwa  mataifa  ya  Afrika hayatatekeleza  waranti  huo , umeeleza  waraka  wa ufupisho  wa maamuzi  hayo.

Mwandishi : Sekione  Kitojo / afpe

Mhariri : Thelma  Mwadzaya