1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi wa Somalia wataka kuondolewa kwa vikosi vya kigeni.

Jane Nyingi17 Septemba 2007

Viongozi wa somalia wanaokutana nchini Saudi Arabia wamesema wanataka vikosi vya africa na vile va kiarabu kuchukua mahala pa vikosi vya kigeni vinavyounga mkono serikali ya mpito nchini Somalia.Viongozi hao hata hivyo wamependekeza vikosi hivyo kuwa chini ya usimamizi wa umoja wa mataifa.

https://p.dw.com/p/CB19
waziri mkuu wa Somalia Ali Mohamed Ghedi wapili kushoto, akiandamana na ujumbe alipokuwa akizuru mji mkuu Mogadishu.
waziri mkuu wa Somalia Ali Mohamed Ghedi wapili kushoto, akiandamana na ujumbe alipokuwa akizuru mji mkuu Mogadishu.Picha: AP

Rais wa somalia Abdullahi Yusuf, waziri mkuu Ali Mohamed Gedi na spika wa bunge Adam Mohamed Nur walitia saini makubaliano hayo mbele ya mfalme Abdullah wa Saudia mjini Jeddah, kufuatia wiki nzima ya mkutano wa maridhiano mjini mogadishu uliosusiwa na makundi mengi ya waasi nchini Somalia.

Makubaliano hayo yanawadia siku kadhaa baada ya mkutano wa wapinzani wao nchini Eritrea uliohudhuriwa pia na viongozi wa mahakama za kiislamu ambao walitimuliwa kusini na kati mwa Somalia walikokuwa wakisimamia, kufuatia makabiliano kati yao na majeshi ya Ethiopia yakisadiwa na yale ya Marekani.

Serikali ya mpito nchini Somalia imekuwa ikijitahidi kukabiliana na mashambulizi ya mara kwa mara kutoka kwa wafuasi wa mahakama hizo tangu walipotimuliwa katika maeneo hayo december mwaka jana.Hatua hiyo imeyafanya maeneo kadha katika mji mkuu mogadishu kugeuka kuwa ya vita hali ambayo imesababisha ongezeko la wakimbizi.

Mapema mwaka huu ,jumuiya ya africa ilikubali kuwapeleka wanajeshi elfu 8 wa kulinda amani nchini Somalia kuchukua mahala pa vikosi vya Ethiopia vinavyounga mkono serikali kutokana na ongezeko la mashambulizi. Hadi kufikia sasa ni chini ya nusu ya wanajeshi hao wamewasili nchini humo.

Marekani ina wasiwasi kuwa wafuasi wa mahakama za kiislamu huenda wakawapa hifadhi wafuasi wa kundi la kigaidi la al-qaeda katika taifa hilo ambalo limekabiliwa na machafuko tangu kupinduliwa kwa serikali ya dictator Mohamed Said Barre mwaka 1991.

Rais abdullahi Yusuf amelitaka taifa la Saudi Arabia mojawapo ya taifa rafiki mkubwa wa marekani kuchukua jukumu la kuzipatanisha pande zinazozana nchini Somalia.

Saudi arabia taifa linalofahamika sana kutokana na utajiri wa mafuta limefadhili mazungumzo kadhaa ya amani katika mataifa ambayo yamekabiliwa na machafuko kama vile Lebanon,Sudan na palestina.Kuna wasiwasi kuwa Ghasia nchini Somalia huenda zikasambaa hadi mataifa jirani.

Taarifa nyingine ni kuwa watu watatu wameauwa na wengine sita kujeruhiwa kufuatia makabiliano kati ya koo mbili kusini mwa Somalia. Mapigano hayo yalikuwa kati ya wapiganaji kutoka koo ndogo za Biyomal na Eny.Ghasia hizo zilitokana na kuawa kwa naibu kamanda wa polisi.