1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi wawili kwa Urusi

Dreyer, Maja16 Aprili 2008

Mada muhimu hii leo ni kuchaguliwa rais Vladimir Putin wa Urusi kuwa mwenyekiti wa chama cha “Urusi iliyoungana”, vilevile ripoti ya shirika linalotetea haki za binadamu Amnesty International kuhusu adhabu ya kifo China.

https://p.dw.com/p/Dirk
Vladimir Putin alichaguliwa kuwa mwenyekiti wa chama cha "Urusi iliyoungana"Picha: AP

Kwanza kuhusu suala la Urusi. Gazeti la “Süddeutsche Zeitung” limezingatia jina lenyewe la chama, yaani “Urusi iliyoungana” na linasema:


“Jina hili linafaa wakati Warusi walikubali sera za rais bila ya kunung'unika. Lakini hali hii inaweza ikabadilika pale Dmitriy Medwedew atakuwa rais mpya. Kuanzia Mei 7 mwaka huu, Medwedew atakuwa mtu muhimu zaidi nchini Urusi, hata hivyo hatakuwa na mamlaka kuliko mtangulizi wake. Kimsingi rais ana haki ya kumfukuza waziri mkuu, lakini kwa kukubaliwa na bunge la “Duma” tu, ambapo lakini chama cha rais Putin kina uwingi. Kwa hiyo basi mamlaka nchini Urusi yamo katika mikono minne badala ya miwili.”


Tukiendelea na gazeti la “Rhein-Neckar-Zeitung”, pia lina shaka kuhusu ugawaji wa mamlaka huko Urusi. Limeandika:

“Putin anafanya jaribio ambalo matokeo yake hayajulikani. Kiutaratibu anafuata katiba na kuondoka katika wadhifa wa urais baada ya kipindi chake kuishi. Wakati huo huo lakini anataka kushika madaraka na kuongoza nchi akiwa waziri mkuu. Huenda mwanzoni atafanikiwa. Lakini kulingana na katiba ya Urusi, rais ndiye mwenye mamlaka makubwa zaidi. Basi, kama Medwedew atataka kutumia mamlaka haya, kutakuwa na viongozi wawili nchini Urusi.”


Mada ya pili: Shirika la kimataifa linalotetea haki za binadamu, “Amnesty International” katika ripoti yake mpya imesema kwamba watu wasiopungua 470 waliuawa baada ya kuhukumiwa adhabu ya kifo huko China mwaka uliopita. Kuhusiana na hayo, gazeti la “Märkische Oderzeitung” limeandika hivi:

“Ikiwa takwimu hizi ni za kweli, maana yake ni kwamba hata wakati michezo ya Olimpiki itakapoendelea, wafungwa wengine watauawa. Kwa hivyo, inafahamika kwamba baadhi ya wanamichezo wanapoteza fuhara yao, lakini bado si hoja kususia michezo hii huko China.”


Na mhariri wa “Financial Times Deutschland” anaonya kwamba:

“Hata ikiwa ni sawa kuzikosoa sera za haki za binadamu za China, bado ni hatari kubwa kuifanya China kama shetani. Ilikuwa imejulikana kwa muda mrefu kwamba serikali ya China inakandamiza makundi ya walio wachache kama Watibet, inatoa adhabu nyingi za kifo na kutoruhusu uhuru wa vyombo vya habari. Hata hivyo, serikali za nchi za Magharibi ziliamua kwa makusudi kuchanganya ukosoaji na ushirikiano zikitumai kuwa mabadiliko yatafikiwa kwa kukaribiana. Na wakati huo huo zinajua kwamba matatizo mengine mengi duniani hayataweza kutatuliwa bila ya China.”