1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vyama vidogo vinashawishiwa kuchukua upande bungeni.

14 Januari 2008
https://p.dw.com/p/CpSS

Nairobi.

Makundi yanayohasimiana nchini Kenya yameanza kushawishi kupata kuungwa mkono kabla ya kile kinachoonekana kuwa mvutano mkubwa wa ufunguzi wa bunge, huku kukiwa hakuna kinachoonekana kumaliza mkwamo wa kisiasa na kitisho cha kuzuka tena kwa machafuko nchini humo.

Baadhi ya wanafunzi nchini Kenya wamerejea shuleni leo Jumatatu huku kukiwa na udhibiti mkubwa wa polisi , licha ya uwezekano wa ghasia baina ya majeshji ya serikali na waungaji mkono wa upande wa upinzani ambao wanapanga siku tatu za maandamano baadaye wiki hii.

Rais Mwai Kibaki anatarajiwa kuzindua bunge la 10 la nchi hiyo , kiasi cha wiki tatu baada ya kurejeshwa madarakani kwa kipindi cha pili lakini watu wa karibu yake wengi wameanguka katika uchaguzi wa bunge.

Si chama cha PNU cha Kibaki wala chama cha upinzani cha Orange Democratic Movement cha Raila Odinga ambavyo vimepata wingi kutosha bungeni, na kusababisha pande hizo mbili kujaribu kuvishawishi vyama vidogo kujiunga na upande wao katika bunge hapo Kesho. Mchambuzi wa masuala ya kisiasa nchini Kenya Evans Manduku amesema kuwa nchi hiyo inakabiliwa na mvutano mkubwa bungeni utakaotamalaki katika masuala ya upendeleo , ulipizaji , na masuala ambayo hayana maendeleo iwapo hali itabaki kuwa kama ilivyo.