1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

WADHIFA WA WESTERWELLE MKUBWA KULIKO UWEZO WAKE?

Martin,Prema29 Agosti 2011

Miongoni mwa mada zilizogonga vichwa vya habari katika magazeti ya Ujerumani leo Jumatatu ni kishinikizo kinachomkabili Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Guido Westerwelle.

https://p.dw.com/p/Rib8
Aussenminister Guido Westerwelle (FDP) gestikuliert am Freitag (12.08.11) in Berlin bei einer Pressekonferenz nach einem Treffen mit dem aegyptischen Aussenminister Mohammed Kamel Amr. Westerwelle und Mohammed Kamel Amr trafen sich in Berlin zu bilateralen Gespraechen. Darueber hinaus diskutierten die beiden Aussenminister nach Informationen des Auswaertigen Amtes die Lage in Syrien. Foto: Steffi Loos/dapd
Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani, Guiido WesterwellePicha: dapd

Basi tutaanza na gazeti la STUTTGARTTER NACHRICHTEN linaloandika:

Waziri Westerwelle, hivi karibuni alisema "Tumefurahi kuona Walibya wamefanikiwa kuiangusha serikali ya Muammar Gaddafi kwa msaada wa operesheni ya kijeshi ya NATO." Bila shaka atafurahi zaidi ikiwa chama chake kitamruhusu kubakia waziri wa nje baada ya kutamka hayo. Kwani mwezi Machi, Ujerumani ilijikuta peke yake kidiplomasia baada ya waziri huyo kutounga mkono azimio la Umoja wa Mataifa kuruhusu operesheni ya kijeshi dhidi ya Libya. Kwa sasa, waziri huyo amenusurika kubakia madarakani. Lakini atathibitishaje kuwa Ujerumani ni miongoni mwa washirika wanaoweza kutegemewa? Hana budi kuhakikisha hilo na pia kuipa kipaumbele kazi yake badala ya kujifikiria zaidi mwenyewe.

Gazeti HESSISCHE-NIEDERSÄCHSICHE ALLGEMEINE likiendelea na mada hiyo hiyo linasema:

Waziri Westerwelle anaezidi kushinikizwa, hakuwa na budi ila kuisifu operesheni ya NATO nchini Libya. Hiyo huonyesha waziwazi kuwa wadhifa aliopewa ni mkubwa kuliko uwezo wake. Wote wanafahamu hilo isipokuwa yeye mwenyewe. Waziri huyo labda, angeondolewa madarakani, lakini tatizo ni kwamba majimbo mawili yatakuwa na uchaguzi hivi karibuni, kwa hivyo kwa sasa, atabakia waziri mpaka atakapoarifiwa upya.

Lakini gazeti la NÜRNBERGER ZEITUNG linaamini kuwa siku za Guido Westerwelle kama waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani, zinakaribia kumalizika. Linaongezea:

Ni kweli kuwa hivi karibuni alijaribu kujipatia heshima kwa kurekebisha msimamo wake na kuisifu operesheni ya kijeshi ya NATO na hivyo kuinusuru kazi yake. Licha ya kuungwa mkono hadharani na kiongozi mpya wa chama chake cha FDP Phillip Rösler, kuna fununu kuwa kiongozi huyo, anataka kumtimua Westerwelle. Na wapo wengi wanaongojea kwa hamu pembezoni, kuchukua nafasi ya Westerwelle.

This photo provided by Andy Weinstein shows some of the 20 beach homes destroyed by surf churned by Tropical Storm Irene along the shore of Long Island Sound in East Haven, Conn., Sunday, Aug. 28, 2011. (Foto:Andy Weinstein/AP/dapd
Uharibifu uliosababishwa na kimbunga IrenePicha: AP

Tukigeukia mada nyingine, gazeti la MANNHEIMER MORGEN linasema hata uharibifu hutoa somo. Linaeleza hivi:

Marekani imeshuhudia kiasi ya vimbunga sita tangu kimbunga Katrin kilipoteketeza mji wa New Orleans hapo mwaka 2005, na kila wakati vimbunga hivyo vilisababisha hasara kubwa ya mali: lakini hata hatua za kuzuia mafuriko, zimeimarishwa sawa na utaratibu wa kuhamisha wakaazi. Somo lililopatikana ni kuchukua mapema hatua za kinga badala ya kukaa na kungojea mpaka dakika ya mwisho. Hivyo ndio Wamarekani wanavyojitayarisha. Kwa hivyo, furaha ni kubwa vimbunga vinapopita bila ya kusababisha uharibifu mkubwa.

Gazeti la DRESDNER NEUESTE NACHRICHTEN likiendelea na mada hiyo linasema:

Kimbunga Irene kilichopita pwani ya New York hakijakuwa kikubwa kama ilivyotazamiwa, lakini kimbunga hicho kimetoa fursa nzuri kwa Rais Barack Obama alipoteza umaarufu wake siku za hivi karibuni. Kimempa fursa ya kudhihirisha uongozi wake wakati wa hatari. Si kitu kama kimbunga hicho hakijakuwa kikubwa kama ilivyotazamiwa.