1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wafanyakazi walioko nje ya Phillipennes waingizia nchi hiyo fedha nyingi.

Sekione Kitojo23 Novemba 2007

Kwa mujibu wa uchunguzi wa hivi karibuni wa umoja wa mataifa , mataifa ya Asia yanapata karibu dola bilioni 114 za fedha zinazopelekwa huko na raia zake wanaoishi nje.

https://p.dw.com/p/CSUC

.

Miezi minne iliyopita eric na mke wake Karen waliondoka Philipines kwenda Lebanon ili kutafuta maisha bora kwa ajili ya familia yao. Wakati akiendesha mabasi nchini Phillipines Eric alipata cheti cha fundi umeme ili kuboresha nafasi yake ya kupata ajira nchi za nje. Kazi ni ngumu lakini nahitaji pesa kwa ajili ya watoto wetu, anasema Eric . Tulijitoa muhanga, tukamuacha mtoto wetu wa kiume Philipines kwasababu ya umasikini. Kuna wakati mshahara wa mwezi mmoja hauwezi hata kulipa kodi ya nyumba.

Wafanyakazi wa Kifilipino nje ya nchi ama kama wanavyofahamika OWF wanawakilisha karibu asilimia 23 ya nguvu kazi nchini humo. Upelekaji wa fedha kutoka kwa wafanyakazi hawa ni sawa na asilimia 13 ya pato jumla la taifa la Philipines GDP, kwa mujibu wa utawala unaowasafirisha wafanyakazi wa Kifilipino nje. Utawala huo unakadiria kuwa kuna zaidi ya wafanyakazi 30,000 wa Kifilipino nchini Lebanon. Mwaka jana utawala huo wa makampuni yanayosafirisha wafanyakazi nchi za nje, umeripoti upelekaji wa wafanyakazi wapya 8,000. Tunatoa fedha kwa serikali yetu, amesema Eric.

Hapo Novemba 18 , idara ya kazi na uajiri ilitangaza kuwa utaratibu wa kuwapata wafanyakazi wahamiaji kutoka Filipino utaanza tena wakati Lebanon itakapoondoa vikwazo katika marufuku iliyowekwa mwaka jana kutokana na hali ya wasi wasi nchini humo. Chini ya sheria mpya , wafanyakazi wahamiaji kutoka Filipino watapelekwa tu Lebanon iwapo watalipwa mshahara wa kima cha chini cha dola 400 kwa mwezi. Kwa hivi sasa kiwango cha mshahara ni dola 200 kwa mwezi kwa Wafilipino, dola 100 kwa Waafrika na dola 150 kwa mwezi kwa Wasri lanka. Ofisi ya wafanyakazi wanaofanyakazi nje ya nchi nchini Sri Lanka , wanakadiria kuwa kuna zaidi ya Wasri lanka wanawake 86,000 walioajiriwa kama wafanyakazi wa nyumbani nchini Lebanon. Ni kundi kubwa kabisa la watu kutoka nje wanaofanyakazi nchini humo. Bernadette , mama wa mtoto mmoja mwenye umri wa miaka 32 kutoka Sri lanka , alikuwa anahitaji uwezo wa kumtunza mwanae wa kike. Nafasi aliyoiona ilikuwa kufanyakazi nje ya nchi. Kwa zaidi ya miaka mitatu amekuwa akifanyakazi nchini Lebanon kama mfanyakazi wa nyumbani. Kila siku Bernadette anaamka saa 12 asubuhi na kufanyakazi kwa muda wa saa 18 za kazi ngumu.

Sri Lanka imepokea kiasi cha dola bilioni 4 kutoka kwa wafanyakazi walioko nje ya nchi hiyo mwaka jana. Benki kuu ya Sri Lanka imeripoti kiasi cha asilimia 7.4 katika ukuaji wa uchumi mwaka jana , kwa kiasi kikubwa kutokana na fedha kutoka nje ambazo zimeingia katika huduma zinazohusiana na teknolojia, ujenzi wa nyumba na viwanda vya nguo.