1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahariri watoa maoni juu ya Tarik Aziz.

Abdu Said Mtullya27 Oktoba 2010

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani leo wanatoa maoni juu ya hukumu ya kifo iliyotolewa kwa Tarik Aziz.

https://p.dw.com/p/Ppoa
Tarik Aziz, aliekuwa mwakilishi muhimu wa utawala wa dikteta Saddam Hussein.Picha: AP

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani leo wanatoa maoni yao juu ya hukumu ya adhabu ya kifo iliyotolewa kwa Tarik Aziz aliekuwa mwakilishi muhimu wa utawala wa Saddam Hussein.
Gazeti la Frankfurter Allgemeine linatilia maanani kwamba Aziz aliepewa adhabu ya kifo kwa kunyongwa ni mtu aliefikwa na bahati mbaya nyingine kwenye msiba.

Gazeti hilo linaeleza kuwa hata ikiwa Tarik Aziz hakuwa na hatia, mtu anaweza kutuhumu kwamba utawala wa sasa nchini Irak wa Waziri Mkuu Nuri al Maliki unaodhibitiwa na washia unatumia sheria za mshindi!
Mhariri wa gazeti hilo pia anatilia maanani kwamba Tarik Aziz ni mtu mwenye umri wa miaka 74 na pia ni mgongwa sana,na kwa hiyo ingelikuwa bora kumwacha afie jela!

Mhariri wa Süddeutsche Zeitung pia anazungumzia juu ya adhabu ya kifo iliyotolewa kwa Tarik Aziz kwa kueleza kwamba Aziz alikuwa mbeba bango wa Saddam Hussein katika mambo ya kidiplomasia. Kutokana na umahiri wake alimwezesha dikteta Saddam Hussein kuwa na sauti duniani.

Lakini mahakimu jana walimwona Aziz kuwa ni mtu mwengine,na siyo mwanadiplomasia. Walimwona kuwa ni mwakilishi wa mfumo wa kidikteta, na walimwona kuwa ni mtu aliewaandama wapinzani wa kisiasa na jamii na dini za wachache.Kwa hiyo adhabu ya kifo aliyopewa ni hatua ya kuuadhibu utawala aliokuwa anauwakilisha.Na gazeti la Münchner Merkur linasema , adhabu aliyopewa Tarik Aziz ni hatua ya kulipiza kisasi.

Mhariri wa gazeti la Flensburger Tageblatt anazungumzia juu ya msimamo wa Kansela wa Ujerumani Angela Merkel kuhusu mkataba wa Umoja wa Ulaya wa kudhibiti nidhamu ya bajeti za nchi wanachama wa Umoja huo. Mhariri huyo anaeleza: kutokana na hali ya kutoridhika miongoni mwa wajerumani nyumbani na kutokana na washirika wengine katika Umoja wa Ulaya kutoridhika, inaekelea ,Kansela Merkel amepoteza dira ya hisia.Nyumbani ameshindwa kuenda sambamba na watu wake na kwenye Umoja wa Ulaya ameshindwa kuwavutia wadau wengine juu ya lengo lake la kuleta mabadiliko ya mkataba wa Umoja huo.Kwa hiyo katika sera zake hakuna ishara yoyote ya hisia za kuleta imani nzuri miongoni mwa watu.

Mwandishi/Mtullya Abdu/Deutsche Zeitungen/

Mhariri/Josephat Charo/