1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahariri wazungumzia juu ya shambulio la kigaidi mjini Moscow.

Abdu Said Mtullya25 Januari 2011

Wahariri wa magazeti leo wanatoa maoni juu ya shambulio la kigaidi mjini Moscow.

https://p.dw.com/p/102VE
Uwanja wa ndege wa mjini Moscow baada ya mashambulio ya magaidiPicha: picture-alliance/dpa

Wahariri wa magazeti mengi yaUjerumani leo wanazungumziajuu ya shambulio la magaidi kwenye uwanja wa ndege mjini Mosko jana.

Watu 35 waliuawa kutokana na shambulio hilo. Wengine zaidi ya 100 walijeruhiwa.

Mhariri wa gazeti la Südkurier anakumbusha kwamba mwaka jana magaidi walifanya shambulio kama hilo, yaani kwenye kitovu cha shughuli za watu. Mhariri huyo anasema yumkini, lengo la magaidi ni kuvinyamazisha vyombo vya dola na kuwatia hofu wananchi.

Mhariri wa gazeti la Flensburger Tageblatt pia anakumbusha kwamba,kwa mara nyingine damu imemwagika mjini Moscow. Lakini mhariri huyo anautafakari mzizi wa fitina kwa kueleza ; kwa mara nyingine pana tuhuma kwamba waliotenda ugaidi wanatokea katika eneo la Kaukusus ya kaskazini. Anasema jambo moja la pasa kuwa wazi kabisa: kwamba vyombo vya ukandamizaji vya Urusi pia vinafanya kazi kwa njia ya ukatili mkubwa katika Kaukasus ya kaskazini. Watu katika eneo hilo wanaishi na hofu inayosababishwa na wababe wa kivita wanaopingana.

Shambulio la jana kwenye uwanja wa ndege wa mjini Moscow linathibitisha ukweli kwamba,siasa ya mabavu ya Urusi katika eneo la Kaukasus imeshindikana. Mhariri huyo anaeleza kuwa hakuna matumaini kwamba serikali ya Urusi itaibadili sera hiyo, kwa sababu huo ndio msimamo wa waziri Mkuu Putin, anaeamini kwamba dawa ya moto ni moto.Putin anaamini kwamba dawa ya ugaidi ni ugaidi!

Katika maoni yake gazeti la Berliner Morgen Post linasema shambulio la jana mjini Moscow ni mbiu ya mgambo.Watu wanapaswa kuwa macho wakati wote. Hata hivyo,mhariri wa gazeti hilo anaeleza kuwa mashambulio ya kigaidi mara nyingine yanatokea kama majanga ya asili. Hakuna anaeweza kusema kwa uhakika, ni wakati gani na ni wapi yanaweza kutokea.Lakini anaeleza kuwa, mashambulio ya kigaidi aghalabu huwa ni ishara ya muundo wa jamii- ni kwa kiasi gani wanajamii wapo tayari kutumia mabomu katika kuyatatua matatizo yao-au ni kwa kiasi gani wapo tayari kutumia njia za kidemokrasia.

Gazeti la Hannoversche Allgemeine linayazungumzia maafa ya jana mjini Moscow, kwa kuizingatia kauli iliyotolewa na katibu Mkuu wa jumuiya ya kijeshi ya NATO- Anders Fogh Rasmussen kwamba tishio la kigaidi dhidi ya Urusi pia ni tishio dhidi ya nchi za magharibi!


Mhariri wa Hannoversche hakubaliani na kauli hiyo.Anaeleza kuwa njia ya kuutatua mgogoro wa Kaukasus ya kaskazini inaanzia kwenye Ikulu ya Urusi.

Mwandishi/Mtullya Abdu/

Deutsche Zeitungen/

Mhariri/...Mohammed Abdul- Rahman.