1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waislamu nchini Kenya wanataka kuandamana kupinga kukamatwa kwa wenzao.

Sekione Kitojo31 Agosti 2007

Waislamu nchini Kenya walifanya maandamano mbele ya makao makuu ya polisi mjini Nairobi kupinga dhidi ya kile wanachosema ni ,kukamatwa kinyume na sheria na mateso dhidi ya Waislamu wenzao katika harakati za kupambana na magaidi zinazoongozwa na Marekani.

https://p.dw.com/p/CB1b

Katika maandamano ambayo yalihusisha watu wachache kufuatia miezi kadha ya hali ya wasi wasi baina ya Waislamu katika taifa hilo la Afrika mashariki na maafisa ambao wanashutumiwa kuwakamata na kuwashitaki baadhi yao kwa amri kutoka serikali ya Marekani.

Hatutarajii hiki kutokea katika nchi hii. Ni kiasi gani cha nguvu ambazo Wamarekani wanazo katika serikali ya Kenya? Amesema Al-Amin Kimathi, mwenyekiti wa chama cha Waislamu cha kutetea haki za binadamu nchini Kenya.

Maafisa wa ubalozi wa Marekani hawakuweza kupatikana kutoa maoni yao.

Ubalozi wa Marekani mjini Nairobi umesema kuwa Marekani inatia nguvu ufanyaji kazi pamoja na washirika wa kimkoa kupambana na ugaidi.

Msemaji wa ubalozi wa Marekani Jennifer Barnes amesema kuwa ubalozi huo unafanyakazi ili kuchafua juhudi za magaidi mahali popote walipo wanapofanya harakati zao.

Makundi ya kutetea haki za binadamu yanaishutumu Kenya kwa kujihusisha katika shughuli za chini kwa chini za Marekani za kuwakamata watuhumiwa na kuwapeleka mahali pa siri.

Polisi wa Kenya wamewakamata watu kadha katika mpaka na Somalia Januari na Februari mwaka huu baada ya majeshi ya Ethiopia na Somalia kuwaondosha wapiganaji wa Kiislamu kutoka mjini Mogadishu, ambao Marekani inawashutumu kwa kuwa na mahusiano na kundi la kimataifa la kigaidi la al-Qaida.

Makundi ya haki za binadamu yanasema kuwa maafisa wa Kenya wanawapeleka watuhumiwa kadha wa ugaidi kutoka Kenya kwenda katika maeneo ya siri nchini Ethiopia kwa ajili ya kuhojiwa na maafisa wa Marekani. Wanaharakati nchini Kenya wamesema kuwa hakuna hata mtu mmoja ambaye amewahi kushtakiwa katika mahakama yoyote ile.

Tunafahamu kutokana na mfungwa ambaye ameachiwa kuwa ni Wamarekani ambao wanafanya mahojiano haya , na serikali ya Kenya inasaidia kufanikisha hilo, amesema Kimathi.

Katika makao makuu ya polisi , waandamanaji walidai kutaka kujua walipo ndugu wawili ambao wametoweka.

Wamesema kuwa polisi wa Kenya walimkamata mmoja kati ya ndugu hao wawili nchini Somalia , na baadaye Ethiopia, mwezi wa Januari bila ya kumshtaki ama maelezo. Alifanikiwa kuwasiliana na nduhu zake mara moja na kuwaeleza mateso aliyofanyiwa, wanaharakati wamesema.

Polisi walimkamata kaka yake mkubwa wiki iliyopita nje ya msikiti mmoja mjini Nairobi , kwa mujibu wa ndugu zake ambao hawajaelezwa chochote zaidi na wanahofu kuwa anakabiliwa na mateso kama yaliyomkumba ndogo wake.