1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanajeshi wa Ukraine wakimbia mapigano Debaltseve

Elizabeth Shoo18 Februari 2015

Mapigano bado yanaendelea nchini Ukraine na yamejikita zaidi katika mji wa Debaltseve, Mashariki mwa nchi. Hata hivyo mamia ya wanajeshi wanasemekana kusalimu amri na kuondoka mjini humo.

https://p.dw.com/p/1EdY3
Mapigano yaendelea Debaltseve
Picha: Reuters/G. Garanich

Waasi wanaotaka kujitenga Mashariki mwa Ukraine wamedai kuteka asilimia 80 ya mji wa Debaltseve, mji wenye kituo cha reli chenye umuhimu mkubwa. Hata hivyo serikali ya Ukraine imekanusha taarifa hizo. Kwa mujibu wa wizara ya ulinzi ya Ukraine, baadhi ya wanajeshi wametekwa nyara mjini Debaltseve. Nalo shirika habari la kundi la waasi linasema mamia ya wanajeshi wamesalimu amri na kujitoa kwenye eneo la mapigano. Wakati huo huo, waasi wanaondoa silaha nzito kwenye maeneo ambapo amani imerejea.

Umoja wa Mataifa umelaani kuendelea kwa mgogoro nchini Ukraine. Nalo baraza la usalama la Umoja huo limepitisha azimio ambalo linataka pande zote mbili ziheshimu makubaliano ya amani yaliyosainiwa wiki iliyopita. Urusi, iliyopendekeza azimio hilo, imesisitiza kwamba inatamani kuona amani ikirejea Ukraine. Vitali Churkin ambaye ni balozi wa Urusi kwa Umoja wa Mataifa alisema: "Tangu kuanza kwa mgogoro huu, Urusi imetaka pawe na suluhu itakayoletwa kwa njia ya amani. Tumefanya kila tuwezalo kutoa nafasi ya mazungumzo kuhusu masuala ya siasa na katiba na tutaendelea kufanya hivyo siku zijazo."

Putin akanusha kuhusika

Lakini Ukraine pamoja na nchi za Magharibi, kama vile Marekani na Ujerumani, zinainyooshea kidole Urusi zikisema nchi hiyo imejihusisha moja kwa moja katika mgogoro wa Ukraine kwa kutuma wanajeshi kuwaunga mkono waasi na pia kuwapatia waasi hao silaha. Makamu wa rais wa Marekani Joe Biden amekemea kukiukwa kwa makubaliano ya amani na amesema Urusi isipochukua hatua italipa gharama kubwa. Akizungumza katika baraza la usalama la Umoja wa Mataifa balozi wa Ukraine kwa Umoja huo, Yuriy Sergeyev, amesema madai ya Urusi kwamba inachangia mchakato wa amani hayatoshi. "Kama Urusi kweli inataka kuchangia juhudi za kuleta amani Ukraine, lazima iondoe wanajeshi wake wote kwenye ardhi ya Ukraine na iwalazimishe waasi wafuate masharti ya makubaliano ya amani ya Minsk," alisema Sergeyev.

Rais Vladimir Putin wa Urusi
Rais Vladimir Putin wa Urusi asema nchi yake haijaingilia mgogoro wa UkrainePicha: picture-alliance/dpa/A. Zemlianichenko

Serikali ya Ukraine imeyataka mataifa ya Magharibi yaongeze shinikizo kwa Urusi. Lakini rais Vladimir Putin, anayekanusha kupeleka wanajeshi Ukraine, amesema mzozo hautakomeshwa kwa nguvu za kijeshi. Badala yake amewaasa wanajeshi wa Ukraine waweke silaha zao chini. Mpaka sasa mgogoro wa Ukraine umegharimu maisha ya watu wapatao 5,600.

Mwandishi: Elizabeth Shoo/ap/afp

Mhariri: Iddi Ssessanga